LIVE STREAM ADS

Header Ads

RAIA WA SOMALIA WAKUBALIWA KUWA RAIA WA TANZANIA.


Watoto hawa walikuwa miongoni mwa wale waliopokea vyeti vyao

Serikali ya Tanzania imetoa vyeti vya uraia wa Tanzania kwa raia wa Somalia zaidi ya elfu moja na mia tano,ambao kiasili walitokea nchini Tanzania zaidi ya karne tatu zilizopita.

Raia hao ambao asili yao wanasema kuwa ni kutoka kabila la wazigua kutoka mkoani Tanga,walizaliwa na kukulia nchini Somalia huku ikiaminika kuwa wao walitokea nchini Tanzania enzi za biashara ya Utumwa kwa zaidi ya ambapo wamekuwa wakitambulika kama Wasomali wabantu.
Mwandishi wa BBC Erick David Nampesya ambaye alihudhuria halfa hiyo anasema kuwa hatua hiyo ya serikali ya Tanzania inahitimisha miaka zaidi ya ishirini ambayo raia hao wapya wa Tanzania wamekuwa wakiishi kama wakimbizi katika nchi inayoaminika kuwa ndiyo asili yao ambayo mababu zao walichukuliwa na kupelekwa ughaibuni enzi za biashara ya utumwa zaidi ya karne tatu zilizopita.


Raia wa Somalia zaidi ya elfu moja na mia tano walitokea nchini Tanzania zaidi ya karne tatu zilizopita.

Pia wamelishukuru Shirika la umoja wa mataifa linalohudumia wakimbizi UNHCR ambalo kwa miaka zaidi ya 20 limekuwa likiwahudumia kwa chakula na mahitaji mengine yote muhimu kwenye kijiji cha Chogo ambako ndiko walikofikia mnamo mwaka 1992 baada ya kutembea umbali mrefu kutoka Kismayo nchini Somalia wakipitia Kenya haadi Wilaya ya Handeni mkoani tanga.

Raia hao wapya wa Tanzania wamepewa uraia ikiwa ni kwa mujibu wa sheria za Tanzania baada ya serikali ya Tanzania kuwafanyia usajili na kuridhika kuwa hapakuwa na sababu za kuwanyima uraia huku pia kukiwa na kundi jingine la wasomali wabantu 150 ambao bado wanasita kuomba uraia wa Tanzania.

Naye waziri wa mambo ya ndani nchini Tanzania Bwana Mathias Chikawe baada ya kuwakabidhi vyeti vya uraia raia hao aliwataka kujisikia kuwa huru.

Hata hivyo aliwataka kuheshimu sheria za nchi na kutowaruhusu maadui wa nchi kuvuruga amani kwenye kijiji hicho cha Chogo,huku akiwataka kujilinda na matendo ya kigaidi na kutoruhusu kushawishiwa na maadui wanaoweza kutumia njia mbali mbali kama mihadhara ya kidini au kisiasa.

Kwa upande wake mwakilishi wa shirika la umoja wa mataifa nchini Tanzania Bi Joyce Mends Cole anasema jukumu lao kwa raia hao sasa limekamilika baada ya kupata uraia,huku shirika hilo likiwa limewajengea zahanati katika kijiji cha Chogo,shule na kuimarisha mradi wa maji ya kunywa.

Vyeti walivyokabidhiwa raia hao

Baadhi ya raia hao wameeleza kuwa kupewa uraia wa Tanzania ni kama ndoto iliyokamilika ambapo sasa wako huru katika nchi yao ya asili pamoja na kwamba hawakuzaliwa Tanzania lakini hadithi za asili yao kutoka kwa babu zao ziliwafanya wasisahau asili yao.

Wengi wanatumia Kiswahili ambacho ni lugha ya asili ya Tanzania lakini pia raia hao wanazungumza kwa ufasaha lugha ya kizigua na sasa wakiwa wameongezea lugha ya kisomali waliyojifunza ughaibuni nchini Somalia.

Inaaminika kuwa nchini Somalia bado kuna Watanzania wengi asilia wanaoishi nchini humo ambao hawana namna wanayoweza kuja nchini Tanzania ingawa wana hamu ya kufanya hivyo.
Na:bbcswahili

No comments:

Powered by Blogger.