LIVE STREAM ADS

Header Ads

SIKU YA MTOTO WA AFRIKA NA ELIMU ISIYO NA VIKWAZO.

Juni 16 ya kila mwaka Umoja wa Afrika sambamba na washirika wake husherekea siku ya mtoto wa Afrika- au kwa kimombo Day of African Child (DAC ), ikiwa ni kumbukumbu ya mwaka 1976 ambapo waandamanaji wanafunzi wa shule za Soweto Afrika ya Kusini waliandamana kupinga elimu iliyokuwa inatolewa kwa manufaa ya utawala wa kibaguzi wa makaburu. Maandamano hayo yalipokelewa na mikono usio na huruma na masikio yasiyo sikivu ya utawala wa kibaguzi na kusababisha vifo vya mamia ya wanafunzi

“Watu wangu, leo nipo huru nipo huru kwa kuwa sintosahaulika kabisa, siku itatimia ambapo kila mmoja wetu atakuwa huru, huru kutokana na unyanyasaji, huru kutokana na uwoga, huru kutokana na kuuwawa, nyinyi ni vijana wadogo mtaishi hadi kuiona siku hiyo na ata kama sintofanikiwa kuiona siku hiyo nyinyi mnatakiwa kusadiki tu kuwa nitakuwepo siku hiyo, hapa ni nyumbani kwangu, pahala pangu pa kuishi.”

Hayo ni maneno ya muigizaji Sarafina katika filamu ya muziki iliyoyaingiza mauwaji ya Juni 16, 1976 huko Soweto. Inaaminika kuwa maandamano hayo yaliyofanyika miaka 38 iliyopita yalikuwa chachu kwa kiwango kikubwa kuuangusha utawala wa kibaguzi nchini humo.

Mwaka 1991 Baraza Kuu la Umoja wa Afrika lilipitisha azimio na kuifanya Juni 16 ya kila mwaka kuwa ni siku ya kuadhimisha siku ya mtoto wa Afrika. Siku hii inatoa nafasi kwa wadau wote wa haki za watoto, zikiwamo serikali mbalimbali, mashirika yasiyo ya kiserikali na ata jumuiya za kimataifa kuyatazama kwa kina matatizo yote yanayowakabili watoto katika bara letu la Afrika".

Kwa mwaka huu yaani 2014 Umoja wa Afrika umetaja lengo Kuu la Siku hii ni kuzitaka serikali zote barani humu kutekeleza majukumu yake ya kuhakikisha watoto wanapata haki ya kupata elimu bora kulingana na mikataba mbalimbali juu ya haki za mtoto ya kimataifa inayosema.

Pakiwa na kauli mbiu,”KUPATA ELIMU BORA NA ISIYO NA VIKWAZO NI HAKI YA KILA MTOTO.” Sio kusema kuwa haki zingine za mtoto zinazikwa katika kaburi la sahau bali Umoja wa Afrika umeziambatanisha haki zingine katika malengo mahususi kwa mwaka huu.

Kulingana na ripoti ya hali ya mtoto wa Afrika iliyotolewa miaka minne iliyopita ilibainisha kuwa elimu katika mataifa mengi ya bara hili imezingwa na matatizo mengi yakiwamo wanafunzi wengi wanaomaliza shule kutokuwa na uwezo wa kutosha kulingana na elimu yao, huku wanafunzi wengi wakiacha masomo kwa sababu mbalimbali zikiwamo mimba, na kukosekana kwa umakini wa kutiliwa mkazo kwa elimu ya awali ambayo inamjenga mtoto katika kupata elimu ya msingi.

Miaka miwili baadaye, yaani mwaka 2012 ripoti juu ya malengo ya milenia ilibanisha kuwa mataifa mengi yaliyo kusini mwa Jangwa la sahara wanafunzi kuacha masomo limekuwa jambo la kawaida huku wanafunzi wengi kutoka familia masikini wakiwa wahanga wakuu. Umoja wa Mataifa kwa upande wake unaungana na Umoja wa Afrika katika masuala haya wakati tukiukaribia mwaka 2015, kama anavyothibitisha katibu mkuu wa Umoja huo, Ba Ki Moon.

“Kupitia matukio duniani kote, tunaadhimisha siku 1000 kuelea kufanikisha malengo ya milenia, malengo ya milenia ni mojawapo ya mbinu kubwa ya kufanikisha kupambana na kuondoa umasikini katika historia ya dunia, hivi sasa nusu ya umasikini imepungua ulimwenguni, wasichana wengi sasa wanapata elimu,vifo vya watoto vimepungua, tunayadhibiti magonjwa yanayoua watu wengi na kadhalika lakini akinamama wengi wanafariki wakati wakijifungua wakati tunazo njia za kudhibiti hali hiyo, pia jamii nyingi zinakosa huduma ya udhibiti wa majitaka, familia nyingi zimeachwa nyuma katika hili, tuna siku 1000 za kuondoa hali hiyo, siku 1000 za kuongeza kasi ya kudhibiti hali hiyo.”

Katibu Mkuu wa umoja wa Mataifa pia aliongeza kuwa zipo njia nne za kufanikisha hali hiyo. Moja kufanikisha mafanikio kwa mbinu mkakati iliyolengwa katika huduma za nishati, udhibiti wa majitaka, afya na Elimi.


Mtoto akitafakari
Zaidi ya hayo kuwawezesha wanawake na wasichana ambao watasaidia kuongeza matokeo mazuri katika nyanja zote, Pili kuweka shabaha kubwa katika sera, hasa maeneo hatarishi ambayo yaliwakwamisha hapo awali japokuwa kulikuwa na jitihada kubwa, tatu, kufanya matumizi sahihi ya fedha kulingana na bajeti husika na siyo kufuja, huu ni wakti wa kujifunga mikanda hatuwezi kufanya matumizi sahihi katika hali hatarishi.

Pia katibu Mkuu huyo alisema, tujitahidi kutia shime katika jitihada za kimataifa, kuanzia serikalini juu hadi katika ngazi ya chini kabisa itaweza kuleta mabadiliko, fanyeni sasa mlete mabadiliko kwa kuongeza kasi wakati tukikaribia mwaka 2015 katika changamoto za maendeleo kuyafikia malengo ya milenia. Malengo haya ya milenia yanasadiia kuleta umoja, yanatia msukumo na kuubadilisha ulimwengu, katika siku 1000 zijazo mafanikio yawe kwa asilimia 1000.

Kiukweli ulimwengu umekuwa na juhudi tele za kumkomboa binadamu na changamoto zote zinazomkabili lakini kubwa ni kwa kila mzazi kutekeleza majukumu yake ipasavyo kwani jitihada zinaanzia mbali kidogo na zinaishia katika ngazi ya familia, Wazazi wanalo jukumu kubwa na kuhakisha wanakuwa chachu ya mabadiliko ya familia, jamiii husika na taifa kwa ujumla. Jamii nzima, walimu na wazazi wanatakiwa kuwa makini na walimu wema kwa watoto wao na kwani mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.

Methali hii inanikumbusha wachekeshaji Lukas Mhavile maarufu kama Joti na Slivery Mujuni au maarufu kama Mpoki ambao wanaigiza kupitia luninga yetu ya TBC1 walipoingiza jinsi baba alivyokuwa akimtuma binti yake Somoe kumuwashia sigira na baadaye binti huyo anakuwa mvutaji wa sigara.

Mchezo huo unaonyesha wazi kuwa baba hakuwa makini na hivyo hakutimiza wajibu wake ipasavyo. Wajibu wa kila mzazi kutafakari mchango wake kwa familia yake wakati Waafrika tukisherekea siku ya mtoto wa Afrika.

Inawezekani wazi kuwa makaburu wa mwaka 1976 kule Soweto waliosababisha madhila kwa watoto walioandamana kwa siku ya leo katika jamiii zetu makaburu hao wanaweza kuwa ni mimi na wewe-kutokana na vitendo vyetu tunavyofanya. Kwa hakika mtoto wa Afrika ni mtoto kama alivyo mtoto kutoka mabara mengine iwe Ulaya , Amerika au Asia. Mshairi Eku MC Gred aliwahi kuzitaja sifa za mtoto wa Afrika katika mojawapo ya mashairi yake.

                                      
                                Watoto wakitabasamu huku wakiwa na matumaini makubwa maishani mwao.
"Mimi ni mtoto wa Afrika, mimi ni mtoto wa Afrika, nimezaliwa nikiwa na rangi ya chokleti inayongaa na inayoonekana kwa kukoza sana, nina sifa kubwaa, nina vipaji tele mimi ni mtoto wa Afrika. Mara nyingi nimekuwa nikifanyiwa hisani, kesho yangu ni ya majaliwa tu, nikipewa zawadi ya maisha tu, nikipewa ndoto na mlango wa mafanikio, nitashinda tu, kwani mimi ni mto wa Afrika. Usiyafiche madhaifu yangu, nielekeze pale nilipokosea, nipo kama binadamu wengine tu, nielekeze namna ya kuyafikia malengo yangu, nitayafikia tu, mimi ni mtoto wa Afrika. Mimi ni mzawa wa ardhi yenye kila aina ya rutuba yenye kesho yenye mafanikio makubwa, nifundishe elimu mbalimbali, nifundishe tabia njema na nifundishe kazi, pia nifundishe kufikiri kama kinara pahala nilipo, mimi ni mtoto wa Afrika".

Ninaweza kuwa si mtu wa kawaida, niite tu Wiliama Kamkwambwa mgunduzi, nipe maktaba yenye kila aina ya vitabu, nipe uwanja wenye kila iana ya vifaa vya kielectoniki nipe baiskeli mbovu nipe tu uhuru nikutengenezea mashine ya upepe ya kusukuma maji, mimi ni mtoto wa Afrika.

Sisi ni kizazi acha tuwe kama tulivyo, weusi tuliyo na vipaji tele, tunangaa kama taa sisi ni watoto wa afrika tunafanya mambo kwa umahiri mkubwa, mimi ni watoto wa Afrika.” Sifa zilizotajwa na mshairi huyo ni nyingi mno zikimsifia mtoto wa Afrika na kama alivyomalizia katika ubeti wa mwisho kuwa mtoto wa |afrika anasifa tele ambazo kwa hakika hakuna mtoto dunia mwenye sifa zaidi ya hizo.

Siku ya mtoto wa Afrika ni sehemu muhimu ya kutathmini masuala muhimu ya watoto hasa kupatikana kwa elimu kwa watoto wenye ulemavu, watoto wenye vipaji maalumu, watoto wanaoishi katika umasikini wa kutisha kuhakikisha na wao wanapata hudumu muhimu za kuweza kuondolewa katika hali hiyo, yatima na wao kufikiliwa pia, watoto wa vijijini, watoto wanaoishi katika vita na maeneo mengine hatarishi, na ata watoto ambao wanaishi magerezani ambapo mama zao ni wafungwa wanakumbukwa pia.

Nchni yetu tangu mwaka 1991 imekuwa ikifanya maadhmisho ya siku ya mtoto w a Afrika nakumbuka ata mimi niliyekuandikia/kutayarisha makala haya wakati huo nilikuwa mtoto nikiona namna watoto wezangu wakishiriki siku hiyo kwa nyimbo na sherehe nyingi. Tanzania imejitahidi kwenda mbali mno kwa kutazama kwa kina matatizo yote yanayowakabili watoto hasa wakiwa majumbani na shuleni.

Waziri wa sheria na katiba Daktari asha Rose Mingiro ni msimulizi wako namuachia usikani wa makala haya ambatana naye. Basi ni wajibu wa kila mmoja wetu pale alipo kutekeleza majukumu yake ipasavyo kuhakikisha mtoto wa Afrika anapata elimu bora na kuwa raia mwema kwa taifa lake kwa nia moja tu ya kujenga Afrika mpya yenye maendeleo. Basi hadi hapo naufunga ukurasa wa makala haya ya siku ya mtoto wa Afrika tukutane tena mwakani.

Imeandikwa na Adeladius Makwega na Kuhaririwa na Angela Mdungu Kutoka Shrika la Utangazaji Tanzania TBC.

No comments:

Powered by Blogger.