LIVE STREAM ADS

Header Ads

VIJANA 158 WATIWA MBARONI JIJINI MWANZA. KATI YAO 36 WAPANDISHWA KIZIMBANI.


Picha haihusiani na habari.
Vijana 36 kati ya 158 wengi wao wakiwa ni machinga ambao walikamatwa siku chache zilizopita Jijini Mwanza kutokana na Vurugu zilizotokea baina yao na Jeshi la Polisi wakati wakipinga kuondolewa katika maeneo yao ya kufanyia biashara katika Mtaa wa Makaoroboi wamefikishwa Mahakamani kwa ajili ya kusomewa mashtaka yanayowakabili.
 
Vijana hao walikamatwa kufuatia vurugu zilizotokea June 11 mwaka huu baada ya Mgambo wa Jiji la Mwanza kufika katika eneo la Msikiti wa Temple maarufu kama Msikiti wa Wahindi na kuondoa meza na vibanda vyao vya kufanyia biashara hali iliyosababisha vurugu kutokea masaa machache baada ya bomoa bomoa hiyo.

Vijana hao walisababisha vurugu kubwa ikiwa ni pamoja na kuwasha moto katika mitaa ya Makoroboi hali iliyohatarisha usalama wa Msikiti huo wa Wahindi ambao nusra uchomwe moto na vijana hao kabla ya kikosi cha zimamoto kufika na kuuzima moto huo kwa madai kuwa waumini wa msikiti huo ndio wanaosababisha wao wasiruhusiwe kufanya biashara zao karibu na eneo hilo la msikiti.

Hali hiyo iliilazimu jeshi la Polisi, Kikosi cha Kutuliza ghasia (FFU) Mkoani Mwanza kutumia mabomu ya kutoa machozi ili kuwatawanya vijana waliokuwa wamekusanyika katika mitaa mbalimbali ya katikati ya ya jiji la Mwanza na hivyo kusababisha shughuli zote kusimama kwa zaidi ya masaa manne katikati ya Mji.

Akizungumza jana na Radio Metro, Kamanda wa polisi Mkoani Mwanza SACP.Valentino Mlowola amesema kuwa jeshi la polisi litaendelea kushiriana Halmashauri ya Jiji la Mwanza katika kuhakikisha kuwa biashara katikati ya mji zinafanyika katika maeneo ambayo yameruhusiwa kisheria na si vinginevyo.

"Metro Radio iko mjini Mwanza, wewe kama mwandishi wa Mjini mwanza umepita katika maeneo ambayo zamani yalikuwa hayapitiki. Hivi sasa unaona njia zimefunguka, mji uko safi na wale ambao walikuwa wanaleta purukushani wamedhibitiwa na wameanza kuelewa lengo letu lilikuwa zuri kwamba tuweke mji katika hali ya amani na usafi na wanapaswa wafuate maeneo ambayo City Council imeelekeza watu wafanyie biashara…”. Alisema Kamanda Mlowola.

Alipoulizwa kuhusiana na vijana waliokamatwa katika vurugu za machinga zilizotokea jijini mwanza alisema “Siyo vijana kumi waliokamatwa ndugu yangu, waliwakamata watu 158. Katika 158, 36 wamefikishwa mahakamani, hili ni jiji lazima liendeshwe kwa taratibu. Ukiona unashindwa kuendesha maisha yako jijini kwa kufuata taratibu nakushauri hapa sio mahali pako pa kukaa, nenda ziwani kavue, nenda kijijini kasukume jembe au kashiriki katika mambo ya mifugo mifugo huko hapa town tunataka watu ambao wanafuata taratibu…”.Alisema Kamanda Mlowola bila kuainisha kama ambao hawajapandishwa kizimbani bado wanashikiliwa na jeshi hilo ama wameachiwa huru.

No comments:

Powered by Blogger.