LIVE STREAM ADS

Header Ads

JANUARY MAKAMBA ASHINDWA KUFICHA HISIA ZAKE. KWA KAULI HII NYUNDO LA CCM LAWEZA KUMWANGUKIA.



Licha ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwafungia kwa mwaka mmoja makada wake sita kwa tuhuma za kuanza mapema kampeni za kugombea urais mwakani, mmoja wa makada hao,  Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, amekiuka maagizo ya chama chake, kwa kutangaza kwamba ameshafanya maamuzi ya kuwania nafasi hiyo kwa asilimia 90.

Akizungumza katika mahojiano na Idhaa ya Kiswahili ya BBC, London Uingereza juzi usiku, Makamba alisema tayari ameshachukua uamuzi huo, lakini kinachokisubiri kwa sasa ni ushauri wa mwisho kutoka kwa makundi mbalimbali wakiwamo viongozi wa dini na wakubwa wake.

Makamba amekuwa akitajwa kuwa miongoni mwa Makada wa CCM wanaotaka kuwania nafasi ya kusimamisha na CCM kupamabana na vyama vingine kuwania urais wakati wa uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwakani.

Kiongozi huyo kutoka miongoni mwa makundi ya vijana wanaotaka kuwania urasi mwakani, hii ni mara yake ya  kwanza kutamka hadharani kuwa na nia ya kuwania urais, ingawa nyendo zake na kauli zake siku za nyuma zilikuwa zikiashiria jambo hilo.

Nyendo hizo za Makamba na makada wengine watano waandamizi wa CCM wanadaiwa kufanya harakati za chini kwa chini kuwania urais kabla ya wakati, zilipelekea  Februari, mwaka huu, CCM kutoa onyo kali dhidi yao.

Makada wengine waliopewa onyo hilo na Kamati Kuu ya (CC) pamoja na Makamba, ni mawaziri wakuu wastaafu, Edward Lowassa na Frederick Sumaye; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe; Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wassira na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.

Mbali na kupewa onyo kali, makada hao pia walitakiwa kutojihusisha na kampeni au vitendo vyovyote  vinavyoashiria kampeni na watakuwa chini ya uangalizi katika kipindi cha mwaka mmoja.
 Mbunge huyo wa Bumbuli (CCM) kwa muda mrefu amekuwa akishawishi umri wa kugombea urais upunguzwe ili vijana nao wapate nafasi ya kuwania nafasi hiyo. Makamba, kwa sasa ana umri wa miaka 40 kwani alizaliwa Januari 28, 1974.

Novemba mwaka jana, Makamba ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, alisema anatafakari kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2015 kutokana na kuwapo kwa watu wengi hasa ndani ya CCM, wanaomtaka kugombea nafasi hiyo ya juu ya uongozi wa nchi.

NEC ya CCM ilishapiga marufuku wanachama wa chama hicho kutangaza nia ya kuutaka urais kwa maelezaoi kuwa, kufanya hivyo ni sawa na kufanya kampeni kabla ya wakati. Makamba, pia alizungumzia mchakato wa kutengenza Katiba Mpya, ambao kwasasa umekwama katika Bunge la Maalum la Katiba baada ya wajumbe wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kususia bunge hilo.
 
Alisema hadi sasa mchakato huo unaonekana kushindwa kufikia maridhiano na wanasiasa wameshindwa kuwapatia Watanzania Katiba wanayoitarajia. Hata hivyo alishauri kwamba, kama mwafaka utashindwa kupatikana katika Bunge hilo kutokana na mivutano ya wanasiasa, mchakato huo usimamishwe na uchaguzi mkuu ujao ufanyike kwa kutumia Katiba ya sasa ya mwaka 1977.
 
Makamba alikuwa Londoni kuhudhuria mkutano wa sekta ya mawasiliano juu ya namna mpya, maarifa mapya na teknolojia mpya za kuendesha mitandao ulioandaliwa na kampuni ya Macktech na Total Telecom ili kusaidia nchi katika sekta ya mawasiliano.

No comments:

Powered by Blogger.