LIVE STREAM ADS

Header Ads

WASIRA ATOA ONYO KALI KWA UKAWA. ASEMA HAKUNA DAMU ITAKAYOMWAGIKA KISA BUNGE LA KATIBA.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Bunda Mkoani Mara (CCM) Mh.Steven Wasira (Alieshika Mikuki) akimsimika Kamanda wa UVCCM Wilaya ya Nyamagana na Kata ya Butimba Robert Masunya (Aliekaa).



Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Bunda Mkoani Mara (CCM) Steven Wasira amewakemea vikali baadhi ya viongozi wa Kisiasa hapa nchini, wanaosema kuwa Bunge Maalumu la Katiba lisipovunjwa amani ya nchini itavurugika.

Wasira ametoa kauli hiyo Jijini Mwanza wakati akimsimika Kamanda wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Wilaya ya Nyamagana na Kata ya Butimba Robert Masunya, katika Mkutano wa hadhara uliofanyika jumamosi katika Kata ya Butimba.

Zaidi Wasira aliwazungumzia Viongozi wa Vyama vya Siasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA ambayo walisusia vikao vya Bunge Maalumu la Katiba, ambao mara kadhaa wamekuwa wakitoa kauli mbalimbali zinazoashiria umwagaji damu endapo kama Bunge Maalumu la Katiba halitasitishwa kuendelea na shughuli zake.

Amesema wananchi wasitishwe na kauli hizo kwa kuwa amani ni haki ya watu wote kwa mjibu wa sheria, hivyo sheria haiwezi kuwavumilia watu wachache wakaivuruga amani iliyopo, ambapo alibainisha kuwa wanaotishia kumwaga damu ya watanzania dola haitawavumilia kwa mjibu wa sheria.


“Wao ni wachache, lakini kila wanachotaka wanataka kipatikane, eti kikikosekana amani hamna…sasa leo nataka niwapashe kutoka hapa Butimba kwamba amani ni haki yetu wote…watu wa ajabu kabisa…wao wanasema msipovunja bunge mtakiona cha mtema kuni…Mimi nawambia hakuna cha mtema kuni na wao wakijaribu ndio watakiona cha mtema kuni...utamwaga damu, umwage ya nani, kwa kweli kwa sheria ya Tanzania hawaruhusiwi hata kumwaga ya kwao…kwa hiyo tunawaambia hawamwagi damu ya mtu nay a kwao hairuhusiwi kumwagika. Dola itakuwepo kulinda damu ya yote pamoja na wao. Habari ndiyo hiyo…”
                                               
Katika hatua nyingine Wasira aliwataka wananchi kuwa Makini katika kuwachagua viongozi wao ambapo alitoa pole kwa Wakazi na Wananchi wa Jimbo la Nyamagana na Ilemela kwa makosa waliyoyafanya kwa kuwachagua viongozi wa upinzani ambao wameshindwa kuwatumikia vyema badala yake wamekuwa wakiwachochea kufanya fujo na kushiriki katika maandamano mbalimbali.



Wasira alibainisha kwamba Serikali katika Mpango wake wa pili wa Maendeleo imeandaa mikakati mbalimbali itakayowasaidia vijana katika kujikomboa na wimbi la ukosefu wa ajira kwa kuwawezesha vijana wenyewe kujiajiri katika shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo na uvuvi wa kisasa sanjari na uwekezaji katika viwanda ambao utawawezesha vijana kupata ajira zaidi.

Aidha Wasira alitoa rai kwa Vijana kutokubali vijana kutumika kisiasa ambapo alibainisha kwamba katika kuwachagua viongozi wawe makini ili wasije wakarudia makosa kama waliyoyafanya katika Chaguzi za mwaka 2010 ambapo waliwachagua viongozi wasio na busara, huku akiwatolea mfano Mgunge wa Ilemela na Nyamagana ambao wameshindwa kuwatumikia wananchi vyema huku akiongeza kuwa Mbunge kama Wenje alichaguliwa kwa bahati mbaya iliyotokea kama ajali hivyo asithubutu kugombea tena katika uchaguzi ujao.



Kwa upande wake Kamanda wa UVCCM Wilaya ya Nyamagana na Kata ya Butimba Robert Masunga baada ya kuapishwa, aliwashukuru vijana wa UVCCM Wilaya ya Nyamagana kwa imani waliyompa ili aweze kuwatumikia ambapo aliahidi kushirikiana zaidi katika kuwatumikia sanjari na kukiimarisha chama cha Mapinduzi zaidi.

Kabla ya Mkutano huo wa hadhara, Wasira alizindua Mashina mawili ya Vijana wa CCM katika Kata ya Butimba ambayo ni Shina la Pangoni Group na Shina la Vijana Bohari ambapo katika Uzinduzi wa Mashina hayo Wasira aliwachangia vijana hao Fedha taslimu kiasi cha Shilingi Laki Tano kila Moja kwa ajili ya kuwaongezea Mtaji katika shughuli za ujasiriamali wanazozifanya vijana hao.

Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza Herry James (Wa Kwanza kulia) akifuatilia tukio zima kwa Umakini wa hali ya juu.
Wananchi wakimsikiliza kwa umakini Mh.Wasira.
Wananchi wakimsikiliza kwa umakini Mh.Wasira.
Hawa siku hiyo nayo walipewa kadi za CCM na kuwa Makada kamili wa Chama.
Mh.Wasira akijumuika pamoja na wanachama wa CCM kufurahia ngoma ya Ritungu kutoka Mkoani Mara.
Ritungu kutoka Mkoani Mara lilinoga sana.
Kamanda wa UVCCM Wilaya ya Nyamagana na Kata ya Butimba Robert Masunya (Mwenye Joho) akipata ukumbusho na Mtanzaniamedia Blog. Namuona Mtani wangu wa Jembe Mary Francis na yeye alikuwepo pia (asie na jezi za chama).

No comments:

Powered by Blogger.