LIVE STREAM ADS

Header Ads

TANESCO YATOA ONYO KALI KWA WAKAZI WA MKOA WA MWANZA.



Shirika la Umeme nchini Tanesco limetoa onyo kali kwa  wakazi wa Mkoa wa Mwanza
wanaolihujumu shirika hilo kwa kujiunganishia umeme bila ya kufuata taratibu hali inayolisababishia shirika hilo hasara kubwa.
 
Hayo yamesemwa na Meneja wa Tanesco Mkoani  Mwanza Stella Hiza kufuatia kuwepo kwa baadhi ya watu kufanya hujuma  kwa kuiba umeme  na hivyo kuwataka  wenyeviti wa  mitaa kuwa makini katika swala hilo kwani  wanao uwezo  wa kuwabaini watu hao.

“Katika hili  viongozi wa serikali za mtaa hawawezi kulikwepa ni wazi kuwa wanawafahamu fika, watu wanaofanya ujanja huo lakini hawataki kuwasema jambo ambalo linaisababishia shirika hasara” alisema Hiza 

Alieleza wananchi  wanatakiwa kuwa wazelendo kwa kutoa taarifa za wizi wa umeme unaoendelea  kwa baadhi ya watu wasiokuwa waaminifu  jambo litakaloleta ufanisi na kuinua maendeleo ya nchi kwa ujumla.

“Kuna watu wanatumia njia hiyo kujinufaisha wenyewe lakini hali hiyo tunapambana nayo kwa kufanya operesheni mbalimbali sehemu ambazo zinakuwa sugu kwa kujiunganishia umeme usiopitia kwenye mita na kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria” alieleza

Kwa upande wake Ofisa usalama wa Tanesco mkoani hapo Ernest Massawe, alisema suala la watanzania kutokuwa wazalendo linachangia kwa kiasi kikubwa katika uharibifu huku likiruhusu mianya hiyo ya wizi kuendelea kuwepo.

Alizitaja hasara zinaweza kujitokeza kuwa ni pamoja na kuunguliwa nyumba jambo ambalo litaleta hasara  na kusababisha vifo visivyo tarajiwa.

“Baadhi ya wananchi hawana uzalendo wanaweza kuwa wanafahamu watu wanaofanya hujuma hizo lakini hawaoni sababu ya kutoa taarifa wakidhani Tanesco ndiyo inapata hasara. kumbuka hata wewe unachangia kulipa kodi, unaweza kupata ajali za moto kwa kua kiwango cha umeme unaounganishwa hakijapimwa kitaalamu.”alisisitiza Masawe

Mkoa wa Mwanza una wateja takribani elfu 70 waliounganishiwa umeme, huku  maeneo ya milimani yakitajwa kuwa ndiyo yanayoongoza kwa kujiunganishia umeme wa wizi na kwa njia zisizo salama jambo linalosababisha hasara kwa Taifa.
Na Prisca Japhes.

No comments:

Powered by Blogger.