LIVE STREAM ADS

Header Ads

KATIBU WA CCM MKOA WA MWANZA AHITIMISHA ZIARA YAKE WILAYANI MISUNGWI.

Katibu wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mwanza akisalimiana na Wanakijiji pamoja na wanachama wa Chama hicho katika Kijiji cha Fela ulipo Mradi wa Maji Fela wakati alipofika Kijijini hapo kwa ajili ya Ukaguzi wa Mradi huo juzi jumamosi.
Na:George GB Pazzo
Katibu wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu amehitimisha ziara yake ya Siku mbili katika Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza, ambapo pamoja na mambo mengine amekagua miradi mbalimbali ya maendeleo Wilayani humo lengo likiwa ni kujionea utekelezaji wa Ilani ya Chama hicho tangu mwaka 2010/15.

Katika ziara hiyo ambayo ilianza jumamosi ya Mach 28 na kuhitimishwa jumapili ya march 29 mwaka huu, Mtaturu alikagua Mradi wa Maji ulio katika Kijiji cha Fela Kata ya Fela, Ujenzi wa Maabara katika Shule ya Sekondari Sanjo pamoja na Zahanati ya Kijiji cha Nyang’homango Kata ya Usagara.

Akikagua Ujenzi wa Maabara katika Shule ya Sekondari Sanjo, Mtaturu alimtaka Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi kushirikiana na wananchi pamoja na wadau wengine wa elimu ili kuhakikisha kwamba ujenzi wa maabara katika Wilaya hiyo unafanikiwa ili wanafunzi wapate fursa ya kusoma vyema masomo ya sayansi huku akiahidi kuchangia mifuko 30 ya simenti kwa niaba ya Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Mwanza ili kufanikisha ujenzi wa maabara katika shule hiyo ya Sanjo.

Katika Ukaguzi wa Zahanati ya Kijiji cha Nyang’homango aliwapongeza wanakijiji wa Kijiji hicho kwa kufanikisha ujenzi wa Zahanati hiyo huku pia akiwahimiza Viongozi wa halmashauri ya Wilaya ya Misungwi kuwahamasisha wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii CHF kwa lengo la kunufaika na huduma za afya kwa gharama nafuu.

Akizungumza na Wananchi wa Kijiji cha Fela ulipo Mradi wa Maji Fela, Mtaturu alieleza kusikitishwa kwake baada ya Mkandarasi TEC Contructs kupitia mhandisi mshauri KOWI kuukabidhi mradi huo kwa halmashauri ya Wilaya ya Misungwi na hivyo kulipwa fedha zote kabla ya muda wa matazamio wa miezi sita kuisha ambapo Mkandarasi huyo ameondoka na kuacha maji hayawafikii wananchi kutokana na mabomba yanayopeleka maji kwenye tank kwa ajili ya kuwafikia wananchi kushindwa kuhimili kasi ya maji hayo.

Akihitimisha ziara hiyo katika Kikao cha halmashauri kuu ya CCM Wilaya ya Misungwi, Mtaturu aliwataka wataalumu wa halmashauri hiyo kuondokana na fikra potofu pindi wanapoona viongozi wa Chama cha Mapinduzi CCM wanatembelea miradi ya maendeleo kwa kuwa wao ni watumishi wa Serikali inayoongozwa na chama hicho hivyo ni lazima chama kitembelea miradi ya maendeleo kwa ajili ya kujionea utekelezaji wa ilani yake.

Jana jioni Mtaturu aliwasili Wilayani Kwimba kwa ajili ya mwendelezo wa ziara zake katika Wilaya zote za Mkoa wa Mwanza ambapo pamoja na shughuli nyingine anatarajia kuwa na mikutano miwili ya hadhara katika jimbo la uchaguzi la Kwimba pamoja na Sumve.
SOURCE:RADIO METRO FM

No comments:

Powered by Blogger.