LIVE STREAM ADS

Header Ads

UONGOZI WA KAMBI YA KULELEA WAZEE WASIOJIWEZA BUKUMBI WILAYANI MISUNGWI WATAHADHARISHWA.

Baadhi ya Wazee wasiojiweka wanaolelewa katika kambi ya Bukumbi Misungwi Mkoani Mwanza.
Na:George GB Pazzo
Uongozi katika Kambi ya kulelea Wazee wasiojiweza iliyopo Bukumbi Wilaya ya Misungwi Mkoani Mwanza, umetakiwa kuimarisha mahusiano mazuri na wafadhiri mbalimbali wanaojitokeza kwa ajili ya ufadhiri kambini hapo.

Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoani Mwanza Miraji Mtaturu alitoa kauli hiyo jana, alipotembelea Kambi hiyo ikiwa ni katika ziara yake ya siku mbili iliyoanza jana March 28 mwaka huu kwa ajili ya kutembelea Wilaya ya Misungwi kwa lengo la kujitambulisha kwa wanachama, kuzungumza na wananchi pamoja kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Ilani ya Chama hicho katika kipindi cha mwaka 2010/15.

Alisema kuwa amepokea malalamiko kutoka kwa baadhi ya Wazee wanaoishi katika kambi hiyo, kuwa uongozi wa Kambi umekuwa na mahusiano yasiyo mazuri na miongoni mwa wafadhiri katika kambi hiyo ya kulelea wazee Bukumbi hali ambayo imepelekea mmoja wa wafadhiri hao kutishia kusitisha ufadhiri wake.

Aidha Mtaturu aliutaka Uongozi wa kambi hiyo kuwajibika katika majukumu yake kwa lengo la kutatua changamoto ndogondogo zilizopo kambini hapo ikiwa ni pamoja na ukosefu wa umeme kutokana na kukosekana kwa fedha za kununulia luku pamoja na matatizo katika mfumo wa Umeme katika kambi hiyo.

Katika kutatua tatizo la Umeme na chakula kambini hapo, Mtaturu kwa niaba ya Chama alikabidhi shilingi Laki Tatu kwa ajili ya kununua Umeme, Mahindi gunia mbili, maharage kilo 30 pamoja na sukari kilo 50,  huku akimwagiza Afisa wa Kambi hiyo kuainisha matatizo ya mfumo wa umeme yanayopelekea umeme kupotea kambini hapo kwa lengo la kusaidia kuyatatua.

Akizungumza kwa niaba ya wazee waliopo nje ya kambi hiyo, Mzee Fabian Malima (55) alilalamikia Marco Bundala ambae ni Afisa Mfawidhi wa kambi hiyo kutokana na kuwabagua katika suala la matibabu pamoja na kutowajumuisha katika mgao wa msaada chakula kinachotolewa na wafadhiri mbalimbali kambini hapo, huku Bi.Helena Emmanuel ambae anaishi katika kambini hiyo akitoa shukurani zake kwa Chama cha Mapinduzi kwa kuwajali na kuwapelekea msaada wa chakula.

Afisa Mfawidhi wa Kambi ya kulelea Wazee wasiojiweza Bukumbi Marco Bundala alikana malalamiko yaliyotolewa na Mzee Fabian Malima (55), kuwa amekuwa akiwabagua katika mahitaji ya chakula na matibabu kwa kusema kuwa amekuwa akiwahudumia wazee wote bila kuwabagua wanaoishi kambini ama nje ya kambi, huku akibainisha kuwa hivi karibuni alipokea maelekezo kutoka kwa Viongozi wake kutowajumuiya wazee walio nje ya kambi hiyo katika mgao wa chakula kinachotolewa na wafadhiri.
Msafara wa Katibu wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (hayuko pichani) ukiwa kambini Bukumbi Wilayani Misungwi.
Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (Kushoto) akikabidhi Mahindi gunia mbili, Maharage Kilo 30 pamoja na Sukari kilo 50 katika Kambi ya kulelea wazee wasiojiweza Bukumbi Misungwi Mkoani Mwanza alipotembelea kambini hapo jana. Katikati ni Afisa Mfawidhi wa Kambi hiyo Marco Bundara akiwa pamoja na Katibu wa CCM Wilaya ya Misungwi Donald Magesa.
Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (Kushoto) akikabidhi Mahindi gunia mbili, Maharage Kilo 30 pamoja na Sukari kilo 50 katika Kambi ya kulelea wazee wasiojiweza Bukumbi Misungwi Mkoani Mwanza alipotembelea kambini hapo jana.
CHANZO: METRO FM

No comments:

Powered by Blogger.