LIVE STREAM ADS

Header Ads

HUU NI ZAIDI YA UNYAMA HIVYO HAUPASWI KUFUMBIWA MACHO.

Hawa ni baadhi ya wanakikundi cha Vijana Mhonze ambapo kutoka kushoto ni Katibu wa Kikundi Nelson Jackson, Masaga Budeba, Frank Laurent, Alfred Haroon pamoja na Alex Amos. 
Kikundi hicho kina wanachama 20.
Na:George GB Pazzo
Kikundi cha Vijana Mhonze kilichopo Kata ya Bugogwa Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza kinachojishughulisha na Mradi wa Ufugasi wa Samaki, kimeingia hasara inayokadiriwa kufikia Shilingi Milioni tano baada ya watu wasiofahamika kusadikika kuwa wamemwaga sumu katika moja ya bwawa la samaki la kikundi hicho na hivyo kusababisha samaki waliokuwemo kufa.

Akizungumza jumatatu ya wiki hii kwa masikitiko makubwa huku akionyesha Samaki waliokufa, Katibu wa Kikundi hicho Nelson Jackson alibainisha kuwa tukio la sumu kumwaga katika bwawa hilo lilitokea usiku wa jumapili baada ya watu wasiofahamika kuvunja wigo na kuingia yalipo mabwawa ya samaki ambapo inaaminika kuwa walimwaga sumu ambayo ilisababisha samaki kufa.

“Huu mradi tuliuanza mwezi Novemba mwakani na tulianza na Mabwawa mawili ambayo yote tuliweka samaki 500 na tayari tulikuwa tumeanza uvunaji, hata jumamosi tulikuja hapa tukavuna samaki na kuwauza kiasi cha shilingi 80,000 lakini jambo la kusikitisha jana tulipokuja tulikutana na majanga maana tulikuta samaki wanaelea wakiwa wamekufa”.
Alisema Jackson na kubainisha kuwa hatua hiyo imekisababishia kikundi hasara kubwa.

Aidha alisema kuwa mradi huo umetumia gharama kubwa tangu kuanzishwa kwake ambapo alibainisha kuwa mbali na kuwekeza nguvu kazi yao, Uradi umekuwa ukiwagharimu shilingi 60,000 kila baada ya wiki tatu kwa ajili ya kununua chakula cha Samaki pamoja na gharama za mafuta ambazo wamekuwa wakitumia katika mashine wakati kubadilisha Maji mabwawani.

Jackson alisema kuwa wakati mradi huo unaanzishwa chini ya usimamizi wa Shirika la Maendeleo ya Jamii na kujengeana uwezo  TAHEA lililopo Nyegezi Jijini Mwanza, vijana wote wa Mhonze walishirikishwa ambapo walijiunga takribani vijana 100 lakini vijana hao walikuwa wakijitoa mmoja baada ya mwingine hadi kikundi kilipobaki na vijana 20 ambao waliendelea na mradi huo wa kufuga samaki.

“Wakati huu mradi unaanza vijana wengi wa Mhonze walishirikishwa lakini leo hii tunasikitika kuona kwamba baadhi yao wanatufanyia hivi maana tunaamini kwamba waliomwaga sumu katika hili bwawa hawakutoka mbali, ni vijana wa hapa hapa Mhonze ambao wamekuwa wakishinda vijiweni bila kujishughulisha hivyo napenda kuwaambia kwamba hiki kitendo si kizuri kwani huu mradi ni wetu sote na ni bora wangejiuka pamoja nasi na kutufanyia hivi”.Alisema Jackson.

Kwa Upande wake Evarist Chikanga ambae ni Mwenyekiti wa Mtaa wa Buganda ulipo Mradi huo alikemea vikali tukio hilo ambapo alibainisha kuwa Serikali ya Mtaa huo ilikuwa ikishirikiana bega kwa bega na Vijana hao tangu mradi huo uanzishwe ambapo aliwasihi vijana kujiunga katika shughuli mbalimbali za uzalishaji badala ya kukaa vijiweni bila shughuli yoyote na hatimae kujiingiza katika uharifu.

“Serikali ya Mtaa wangu imekuwa ikishirikiana na vijana hawa tangu mradi huu unaanzishwa na kwa tukio hili kitu ambacho tutakifanya ni kuhakikisha kwamba wale wote waliohusika tunawakamatwa lakini pia tumepata funzo kubwa katika mtaa huu hivyo suala la ulinzi shirikishi nitahakikisha kwamba linaimarishwa zaidi”. Alisema Chikanga.

Afisa Uvuvi Msaidizi Manispaa ya Ilemela Alpha Faustine Paragha alifika eneo la tukio na kuchukua Sampuri ya Samaki waliokufa pamoja na Maji ya bwala linalosadikika kuwekewa sumu kwa ajili ya kupelekwa katika maara ya Uvuvi Nyegezi Jijini Mwanza ili kupata uhakika wa sumu iliyomwagwa bwawani huo.

“Samaki anaweza akafa kwa kukosa hewa aina ya Oxygen lakini hapa ni karibu na Ziwa na kuna maji mengi hivyo ni vigumu samaki kufa kwa kukosa hewa katika eneo hili na kwa kuwa inasadikika ni sumu nitachukua sampuri ya maji na samaki waliokufa kwa ajili ya kuipeleka katika Maabara ya Uvuvi Nyegezi ili kupata uhakika wa sumu iliyomwagwa humu”. Alisema Paragha ambae alisikitishwa na tukio hilo.

Msimamizi wa Vijana kutoka Shirika la Maendeleo ya Jamii na Kujengeana Uwezo Faraji Faustine Benge alisema kuwa Mradi huo wa Samaki wa Vijana Mhonze ulianzishwa chini ya Shirika hilo ukiwa ni miongoni mwa miradi mingine ya Vijana inayosimamiwa na Shirika hilo katika Manispaa ya Ilemela ambayo ni pamoja na Mradi wa Ufyatuaji wa Matofali, Ufundi Cherehani pamoja na Michezo.


“Gharama zote ambazo zimefikiwa tangu kuanzishwa kwa mradi huu ni takribani Milioni tano ambazo kwa sasa tunaona zimeyeyuka kwa sababu ni hasara kubwa iliyopatikana kutokana na tukio hili, lakini sisi kama TAHEA hatuwezi kuwaacha hawa vijana maana tutawakatisha tamaa hivyo tutashirikiana tena na Manispaa ya Ilemela ili kuhakikisha kwamba tunaibua upya tena huu mradi maana bwawa lililoathirika ni moja kati ya haya mawili yaliyopo hapa”. Alibainisha Benge wakati akiwa eneo la tukio.

Ni dhahiri, shahiri kwamba tukio hili ni la kinyama na halipaswi kufumbiwa macho kwa kuwa linakwamisha juhudi za vijana kujiajiri kwa lengo la kupunguza kasi ya ukosefu wa ajira ambao umekuwa ni changamoto kubwa hapa nchini, hivyo ni vyema uchunguzi ukafanyika na wale wote waliohusika wakachukuliwa hatua za kisheria kama alivyoahidi mwenyekiti wa Mtaa wa Buganda.
         Bonyeza HAPA Kutazama Picha

No comments:

Powered by Blogger.