MWENYEKITI WA MTANDAO WA WATOTO MKOANI MWANZA ACHUKUA FOMU YA KUGOMBEA UBUNGE.
Kushoto picha ya juu na Katikati picha ya chini ni Shabani Maganga baada ya kuchukua fomu ya kuwania kugombea Ubunge jimbo la Ilemela Mkoani Mwanza.
Judith Ferdinand
Mwenyekiti Mtendaji wa Shirika lisilo la kiserikali la Mtandao wa Watoto na Vijana Mwanza Shabani Maganga (28), amechukua fomu ya kugombea ubunge jimbo la Ilemela kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM),katika uchaguzi wa mwaka huu.
Maganga ambae amebobea katika masuala ya utatuzi wa matatizo yanayoikabili jamii, pia amewahi kushika nyadhifa za uongozi katika nyanja mbalimbali ikiwemo Mwenyekiti wa Baraza la Watoto la Jamhuri ya Tanzania, Mwenyekiti baraza la watoto mkoa wa Mwanza pamoja na uongozi mbalimbali akiwa ni mwenye elimu ya chuo kikuu.
Akichukua juzi fomu hiyo, Maganga alisema lengo liliopelekea kujikita katika kinyanganyiro cha kuwania ubunge ni kutokana na changamoto zinazokabili jimbo hilo, licha ya kuwa na rasilimali nyingi ambazo zingeweza kutatua matatizo hayo.
Alisema kuwa jimbo la Ilemela linahitaji kiongozi anayeweza kutatua matatizo hayo kwa kutumia rasimali zilizopo kwa kunufaisha na kuleta maendeleo kwa wananchi.
Pia alisema amejipima na anamini uwezo wa kuongoza wananchi anao, hivyo ana dhamira ya dhati ya kulikomboa jimbo hilo kwa kugeuza changamoto kuwa fursa na huzuni kuwa furaha kwa kushirikiana na wananchi.
“Hali za wakazi wa jimbo la Ilemela wakiwemo watoto, wazee, vijana na wakina mama, hivyo matatizo yanayokabili jimbo letu hayaitaji Mchina, Mzungu wala Mjapani kuja kuyatatua bali ni Mwanailemela anayejua uchungu wa changamoto hizo atakayebadili huzuni kuwa furaha na changamoto kuwa fursa”. Alisema Maganga.
Hata hivyo aliwaomba wanachama wa CCM kumuunga mkono ili kumsimamisha kuwa mgombea ambaye ataenda kutetea wananchi,kuwasemea matatizo yao, kwani ataki kuwa mbunge wa kujinufaisha yeye bali kulitumikia na kuliletea mandeleo jimbo hilo.
No comments: