LIVE STREAM ADS

Header Ads

+AUDIO. MACHINGA WAITADHARISHA HALMASHAURI YA JIJI LA MWANZA JUU YA BAJETI YAKE 2016/17.

Kushoto ni Mwenyekiti wa Muungano wa Machinga Mkoani Mwanza Said Tembo akiwatazama baadhi ya Vijana ambao ni Machinga Jijini Mwanza.
Halmashauri ya Jiji la Mwanza imetakiwa kupanga vyema mikakati yake ya bajeti ya fedha katika kipindi cha Mwaka 2016/17, kwa ajili ya Makundi ya Vijana na akina Mama, ili kuyasaidia makundi hayo kujiajiri na hivyo kuondokana na tatizo la ukosefu wa ajira.

Mwenyekiti wa Muungano wa Machinga Mkoani Mwanza Said Tembo, ametoa kauli hiyo wakati akizungumzia changamoto ya ukosefu wa maeneo maalumu kwa ajili Wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kwa jina la Machinga Jijini Mwanza, jambo linalosababisha wafanyabiashara hao kuzagaa ovyo mitaani kinyume na taratibu za Halmashauri ya Jiji la Mwanza.

Pamoja na mambo mengine, Moshi Maketa ambae ni Katibu Mkuu wa Muungano wa Machinga Mkoani Mwanza, amesema kuwa Muungano huo unafanya kila jitihada ili kuhakikisha Serikali inatoa mikopo kwa ajili ya Machinga, ili kuwawezesha kujikwamua kiuchumi ikizingatiwa kwamba Sekta ya Machinga imekuwa kimbilio la vijana walio wengi hapa nchini.

Jijini Mwanza, baadhi ya Machinga wanapaza sauti zao na kuiomba Serikali kuiboresha Sekta hiyo, ili kuondokana na Changamoto zinazowakabiri ikiwemo kukosa maeneo maalumu kwa ajili ya kufanyia biashara zao, hatua inayosababisha wakumbane na kadhia mbalimbali ikiwemo kukabiliana na mgambo wa Jiji.

Japo biashara ya machinga si biashara rafiki katika maeneo ya katikati ya Jiji la Mwanza, lakini biashara hiyo imekuwa kimbilio la Vijana walio wengi hususani kutoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa, ambao kila kukicha hufika Jijini Mwanza kwa ajili ya shughuli hiyo huku changamoto mpya ikiwa ni kuanza kuwepo kwa idadi ya watoto wanaojiunga na biashara ya Machinga Jijini Mwanza na hivyo kusababisha watoto hao kukosa haki yao ya kupata elimu.
BONYEZA HAPA KUSIKILIZA

Mmoja wa Machinga akifanya biashara katikati ya Jiji la Mwanza
Baadhi ya Machinga Jijini Mwanza eneo la Mataa
Baadhi ya Vijana Machinga Jijini Mwanza
Baadhi ya akina Mama wanaojishughulisha na biashara ya Kuuza Mihogo Jijini Mwanza
Mwenyekiti wa Muungano wa Machinga Mkoani Mwanza Said Tembo akizungumza na BMG kama ambavyo alinaswa katikati ya Jiji la Mwanza eneo la Mataa.

No comments:

Powered by Blogger.