LIVE STREAM ADS

Header Ads

Fanya Mambo Haya Saba Ndani Ya Mwezi Huu Mpya.

Kwanza nakupa pongezi na hongera kwa kuwa pamoja katika kumaliza Mwezi uliopita wote wa pili; ambao umeisha tangu hapo jana na sasa tumeingia mwezi mpya wa tatu. Kumbuka Utukufu na Nguvu ni kwa Mungu aliyetupa tena nafasi ya kuingia na kuuona tena mwezi huu mpya wa tatu tuliouingia hii leo.

Na hivyo basi, leo napenda kukushirikisha mambo muhimu ambayo ningependa uyafanye ndani ya mwezi huu mpya tunaouanza hii leo, na hasa kama unahitaji kufanikiwa katika Malengo na ndoto yako uliyonayo ndani ya mwaka huu 2016.

Kumbuka kila mwezi ndani yake ni mfano wa MIMBA ambayo umeibeba wewe muhusika, na ambayo ni muhimu ujue unatakiwa mwezi usiishe umekwishajifungua. Mimba ya kukusukuma kwenye kufanikisha malengo yako ya mwaka mzima na hatimaye kufanikisha ndoto zako ulizonazo maishani mwako.

Suala sio kumaliza mwezi; Bali swali la muhimu la kujiuliza ni Je, mwezi unapoisha unakuwa umefanikisha mambo mangapi yanayokupa nafasi ya kutimiza ndoto yako nzuri uliyonayo maishani mwako? Hilo ni swali muhimu na la msingi unalopaswa kujiuliza kila mara kabla na baada ya kuingia mwezi mwingine.

Kama hukubahatika kufanikisha mambo yako mengi ndani ya mwezi uliopita; na yawezekana hadi sasa hujui utafanya nini. Nakusihi fanya yafuatayo ili yawe sehemu kubwa ya kukusaidia kufanikiwa katika Malengo yako ndani ya mwezi huu wa 3 tuliouanza hii leo, na ili usikosee tena kwa mara nyingine kufikia malengo yako.

1:Tafuta jambo moja la kusimamia na kufanya mwezi huu mzima.
Usijaribu kufanya kila kitu, utafeli kwa kufanya kila kitu. Chagua jambo moja la kukusaidia kukupeleka katika kutimiza ndoto yako kiujumla ndani ya mwezi huu. Hii itakujengea msingi mzuri na msimamo mwema wa kufikia katika mafanikio makubwa unayoyahitaji.

Utafiti unaonyesha wazi watu wengi wenye kujaribu kufanya kila jambo wanaloona kwao linamanufaa na kuacha kusimamia jambo moja; huwa wanajikuta wanakosea mara kwa mara na hatimaye hata kushindwa kupata kitu kikubwa walichokuwa wakitegemea kupata katika maisha yao.

2:Orodhesha watu si chini ya watano ambao unapaswa kukutana nao haraka; ili kukusaidia katika kufikia malengo yako.
Hakuna mafanikio yanayoweza kufikika kama hayatojengwa kwenye msingi wa kushirikiana na wengine. Unahitaji watu kila siku wa kukusaidia kutimiza na kufikia ndoto yako kubwa uliyonayo maishani mwako. Kama hautoona umuhimu wa kushirikiana na watu fahamu utakuwa unakosa nafasi kubwa ya kufika haraka unapotaka kufikia.

Kwa kufahamu jambo hili zaidi; soma makala hii ya Unahitaji watu sahihi wa kukubeba ili Kufikia katika Mafanikio makubwa itakupa ufahamu zaidi.

3:Orodhesha kiwango cha rasilimali fedha na muda unachokihitaji kila siku ili kufikia malengo yako ya mwezi huu mzima.
Usitumie muda wako na fedha yako vibaya; jiwekee bajeti ya mwezi huu mzima; ili kukupa nafasi ya kutembea katika matumizi yaliyo ya muhimu na ya lazima tu katika eneo hili la fedha na muda. Fedha na Muda ni rasilimali muhimu sana ambazo zinaweza kuwa sehemu kubwa ya kumsaidia mtu kufikia katika malengo mengi yanayohitaji rasilimali hizi.

Wewe binafsi unajua na kufahamu ya kuwa; karibu asilimia kubwa ya malengo mengi ya watu au yako yanahitaji fedha na muda wa kutosha ili kuweza kuyatimiza kwa uaminifu na ili uweze kuyafikia pasipo kigugumizi chochote mbele yako. Ingawa bado utahitaji furaha na amani pia kama mambo muhimu zaidi.

4: Badili muda wako wa kulala na kuamka.
Nakusihi uache tabia ya kuchelewa kulala, kwa kufanya hivyo ni lazima utachelewa kuamka pia. Na hata kama si kuchelewa kuamka fahamu unaweza kushindwa kufanya mambo yako vizuri katika siku yako inayofuata mbele yako.

Jiwekee ratiba nzuri itakayokuongoza katika muda wako wa kulala na kuamka mapema; ili uweze kujiendesha vizuri katika eneo hili na zaidi sana ili uweze kujisaidia binafsi kwenye suala la afya na nguvu za kutimiza ndoto yako. Kumbuka kuwa masaa yako unayoyatumia kulala ndio yanayoamua uwezo wako wa kufanya kazi katika siku inayofuata. Kama hutolala usingizi wa kutosha fahamu kesho yake itakuwa ngumu kufanya kazi vizuri kwa sababu utakuwa umechoka.

Hivyo hivyo kwa upande wa pili. Kama utapata muda mrefu wa kupumzika na kulala vya kutosha utakuwa umesaidia mwili na akili yako kujituma zaidi katika siku inayofuata mbele yako. Ushauri wangu kwako ni kuwa, hakikisha unatekeleza jambo hili kuanzia leo hii ili uweze kuona matunda mazuri juu ya kazi zako na afya yako.

5:Zingatia kula chakula kilicho bora ambacho kinaweza kuwa msingi mzuri wa kukufanya uwe na afya bora na nguvu ya kukusaidia katika kutimiza ndoto na malengo yako uliyonayo.

Chakula unachokula ndio kinaamua afya yako na nguvu zako za mwilini za kukusaidia katika kutimiza ndoto na maono yako mazuri uliyonayo. Hakikisha unapangilia mlo wako na chakula unachotumia ili kukupa nguvu ya kutumikia maono na kusudi la kuwepo kwako hapa duniani.

Tumia vyakula vizuri visivyo na mafuta mengi na vinywaji visivyo na kokeini nyingi; usitumie vinywaji hivi mara kwa mara au uviache kabisa, vinywaji kama vile soda, vinywaji vya kuongeza nguvu (energy drinks), nakadhalika; vinavyoweza kuwa hatari kwa afya yako na zaidi kukusababisha wewe kushindwa kutumikia na kufikia malengo na ndoto zako ulizonazo.

6:Badili misimamo na tabia mbaya zisizofaa.
Tabia zinazokuzuia katika kufikia mafanikio makubwa. Zipo tabia zinazoweza kuwa kizuizi kikubwa cha kumsababisha mtu kutokuweza kufikia katika mafanikio makubwa ya kutimiza ndoto yake. Na zaidi sana watu wengi wamekuwa na tabia hizi zinazokuwa kizuizi kwa upande wao wa kufikia mafanikio.

Fatilia makala hii ya Tabia 20 zinazozuia watu wengi kufikia katika mafanikio makubwa utaelewa tabia hizo; soma kisha chukua hatua ya haraka ya kubadilika kutoka katika tabia hizo ili uweze kufikia katika mafanikio yako unayohitaji.

7:Soma vitabu 2 hadi 4 ndani ya mwezi huu.
Hakuna mafanikio makubwa nje ya kutoa muda wako kila siku kwa ajili ya kujifunza mambo mapya yanayoweza kuwa msingi mzuri na mwema wa kukusaidia kufikia maono na ndoto zako ulizonazo. Jiulize unapendelea kusoma mambo gani; kumbuka kuwa yale unayoyasoma ndio yanayokujengea tabia tunayoiona hii leo huku nje; jiulize swali kama unasoma na kufatilia zaidi mambo ya udaku; Je, yanakusaidia vipi katika kufikia maono na ndoto yako uliyonayo moyoni mwako?

Hivyo basi, hakikisha unasoma mambo mazuri au vitabu vyenye maudhui mazuri ya kukujenga kitabia na kukusaidia katika kufanikisha ndoto yako na kusudi la kuwepo kwako hapa duniani. Achana na kusoma habari za udaku tena za maisha ya watu ambao asilimia kubwa wapo kwa ajili ya kuigiza zaidi, kuliko kuonesha uasilia wa mafanikio yao ya kweli.
Hadi kufikia hapo nakutakia mafanikio mema ndani ya mwezi huu tuliouanza; kumbuka ukitii na kufaata mambo yote niliyokuandikia hapo juu, naamini utakula mema yote ya mwezi huu, na zaidi utaona mafanikio katika kila jambo unaloligusa kulifanya.
Shukrani kwa ccbanttz Consultant.

No comments:

Powered by Blogger.