VYOMBO VYA HABARI VISIVYO NA WAKALIMANI KITANZINI.
Serikali imevitaka vyombo vya habari nchini hasa vya luninga hadi kufika mwezi machi 2017, kutumia wakalimani wa lugha ya alama katika kutoa taarifa za matukio muhimu zikiwemo taarifa za habari.
Akizungumza jana katika maadhimisho ya kimataifa ya watu wenye ulemavu Waziri wa Sera, bunge, kazi, vijana na ulemavu , Jenista Mhagama, alisema pindi muda huo utakapofika watakwenda kufuatilia matakwa ya sheria namba 9 ya mwaka 2010 inayovitaka vyombo vyote vya habari kuhakikisha vinatoa lugha ya alama ili kuwafanya watanzania wenye ulemavu waweze kufuatilia matukio mbalimbali yanayotokea Tanzania bila kuachwa nyuma.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Shirikisho la vyama vya watu wenye ulemavu (SHIVYAWATA), Ummy Hamisi Nderiananga, alizitaka taasisi ambazo zilizoanzishwa kwa lengo la kuwasaidia watu wenye ulemavu na hazifanyi hivyo kufungiwa kwani zimekuwa zikifanya mambo yake kwa kupitia mgongo wao.
Nae Katibu Tawala wa halmashauri ya manspaa ya Ilala, Edward Mpogolo alisema kuwa baadhi ya wazazi na walezi wa watoto wenye ulemavu katika mkoa wa Dar es Salaam wanadaiwa kuongoza kwa kutelekeza watoto wao katika shule maalumu za walemavu hasa zilizopo katika wilaya ya Ilala.
Mpogolo aliyasema hayo wakati akieleza changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu katika mkoa wa Dar es Salaam.
“Dar ina shule za watu wenye ulemavu nne, tatu zipo Ilala. Wazazi na walezi hao wamekuwa wakiwapeleka watoto katika shule hizo kwa lengo la kupata elimu kisha kuwatelekeza,” alisema.
No comments: