LIVE STREAM ADS

Header Ads

Pumzika kwa amani mzee Majuto

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Na Emmanuel Shilatu
Nimepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa za msiba wa msanii nguli na bingwa wa tasnia ya sanaa za uigizaji na vichekesho, Amir Athuman almaarufu "King Majuto" kilichotokea usiku wa Agosti 8, 2018 katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu kutokana na maradhi yaliyokuwa yakimsumbua.

Kifo hiki kimenikumbuka miaka ile ya zamani alipoanza kuwika na msemo wa hamsini, hamsini mia akiwa na muigizaji mwenzake mkongwe marehemu mzee Small. Kwa wasiomjua vyema King Majuto alizaliwa mwaka 1948 jijini Tanga na kusoma shule Msambwini mkoani Tanga. Alianza kuigiza mwaka 1958 akiwa na umri wa miaka tisa akiigiza katika majukwaa.

Mzee Majuto maarufu kama King Majuto ni mtunzi, muigizaji, mwandishi wa mswada. Pia mzee Majuto ni muigizaji wa kwanza kuandaa kazi zake katika mikanda na kuuza akiwa na Tanzania Film Company ( TFC). Kwa sasa King Majuto ni mwigizaji mwenye mashabiki wengi kutokana maonyesho mbalimbali, vichekesho vyake aliyoshiriki. King Majuto ni kipaji halisia cha kuzaliwa cha uchekeshaji kuwahi kutokea hapa nchini. 

Wenzake walikuwa kina Mzee Jongo, Hamis Kitambi, Fundi Said (Mzee Kipara) na Mama Haambiliki. Msiba huu ni majonzi makubwa sana kwa familia, wasanii, tasnia ya filamu nchini, wapenzi wa kazi zake za sanaa na Taifa kwa ujumla. Daima tutakukumbuka kwa ufundi, ustadi wa uigizaji wako, vituko vyako, tabasamu lako, upendo wako kwa kila mtu.


Pumzika kwa amani mfalme na bingwa wa vichekesho wa kipindi chote hapa nchini mzee "King Majuto". Inna lillaahi wainna ilaihi raajiuun.

No comments:

Powered by Blogger.