Usajili Rock City Marathon 2018 waanza rasmi
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Na Mwandishi Maalum
Mkuu wa mkoa wa Mwanza Mheshimiwa John Mongella amekuwa
mshiriki wa kwanza kujisajili kushiriki mbio za Rock City Marathon
zinazotarajiwa kufanyika Oktoba 28 mwaka huu katika viwanja vya CCM Kirumba.
Akizungumza kwa niaba ya RC Mongella kwenye hafla fupi
iliyofanyika Setemba Mosi, 2018, Mkuu wa Wilaya Nyamagana Mhe. Dkt. Philis
Nyimbi alitoa wito kwa wadau wa michezo na utalii katika Kanda ya Ziwa
kuhakikisha wanayatumia vizuri mashindano hayo katika kutangaza fursa na
vivutio vya utalii na kukuza mchezo wa riadha.
Pia aliwapongeza waandaaji wa mbio hizo kampuni ya Capital
Plus International na kutoa rai kwa waandaaji
hao kushirikiana na viongozi wa mchezo wa riadha nchini kuhakikisha
wanakuwa na mkakati wa kudumu unaolenga kuwaandaa washiriki kutoka ndani ya
nchi ili waweze kuleta matokeo mazuri dhidi ya washiriki kutoka mataifa ya nje.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa mbio hizo, Zenno Ngowi
aliwasihi washiriki wanaotoka ndani ya nchi kufanya maandalizi ya kutosha
kutokana na ushindani mkubwa unaotarajiwa kutoka kwa washiriki wa nje ya nchi
ambao, kwa mujibu wake wameonesha mwitikio mkubwa wa kushiriki katika mbio
hizo.
Alivitaja vituo vitakavyohusishwa katika usajili huo kuwa ni
pamoja na Igoma, Buzuruga, Airport Mwanza, Rock city mall, Chuo Kikuu cha Saut,
Nyegezi Stand, Mwanza hotel, Nyamagana Stadium, Dampo pamoja na Nyakato.
Alisema usajili huo pia utahusisha ofisi zote za riadha mikoa ya Geita, Simiyu
na Shinyanga.
Alisema usajili huo utahusisha mbio za km 42 kwa wanaume na
wanawake, Kilomita 21 kwa wanaume na wanawake, km 5 kwa washiriki kutoka kwenye
mashirika (Corporates) na walemavu wa ngozi, km 3 kwa wazee wenye umri kuanzia
miaka 55 na kuendelea pamoja na km 2.5 kwa watoto wenye umri wa miaka 7 hadi
10.
No comments: