LIVE STREAM ADS

Header Ads

Mbunge Dkt. Ashatu Kijaji aeleza utekelezaji wa Ilani ya CCM jimbo la Kondoa

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Mbunge wa jimbo la Kondoa mkoani Dodoma, Dkt. Ashatu Kijaji amewahimiza wakazi wa jimbo hilo kuendelea kushirikiana na serikali pamoja na wadau mbalimbali katika kutekeleza shughuli na miradi ya maendeleo ikiwemo elimu, afya, maji pamoja na miundombinu.

Dkt. Kijaju alitoa rai hiyo jana wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi CCM ya mwaka 2015/20 katika kipindi cha miaka mitangu tangu achaguliwe kuwa mbunge wa jimbo hilo, kwenye Mkutano Mkuu Maalum wa chama hicho wilaya ya Kondoa.

Katika sekta ya maji, Dkt. Kijaju alisema visima 56 vimechimbwa na kukarabatiwa kwa fedha za serikali na wadau wa maendeleo ambazo ni shilingi 1,808,075,696 hatua ambayo imesaidia wakazi wa jimbo la Kondoa kuondokana na kero ya uahaba wa maji.

Alisema ujenzi wa vyumba vya madarasa, nyumba za waalimu, vyoo bora, utengenezaji wa madawati, ujenzi wa shule mpya, ukarabati wa shule za zamani pamoja na makambi ya wanafunzi umesaidia kuongeza ufaulu katika sekta ya elimu kutoka asilimia 37 mwaka 2014 katika mtihani wa darasa la saba hadi asilimia 68 mwaka 2017.

Kwa upande wa sekta ya afya, Dkt. Kijaji alisema vituo vipya vinne vya afya vimejengwa huku kituo kimoja cha afya kikifanyiwa ukarabati mkubwa ambapo shilingi bilioni 2.3 zimetengwa kwa ajili ya kukamilisha uboreshaji wa sekta hiyo.

Alipongeza juhudi serikali, wananchi na wadau wa maendeleo zilizofanyika katika kipindi cha miaka mitatu na kufanikisha uboreshaji wa miundombinu ya barabara pamoja na madaraja huku Vijiji vinane vikinufaika na umeme kupitia mpango wa REA II na kwamba Vijiji 73 vinatarajia kunufaika na mpango huo katika awamu inayofuata.

Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali pamoja na wajumbe zaidi ya elfu moja wilayani Kondoa ambapo walifurahishwa na taarifa Dkt. Kijaji ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango wakisema ni mfano bora unaopaswa kuigwa na viongozi wengine.
Mbunge wa Kondoa, Dkt. Ashatu Kijaji (wa pili kushoto) pamoja na viongozi mbalimbali mkoani Dodoma wakiwa kwenye mkutano huo.
Sehemu ya wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalum wa Chama cha Mapinduzi CCM wilayani Kondoa
Mbunge wa jimbo la Bukombe, Mwl. Doto Biteko ambaye pia ni Naibu Waziri wa Madini ni miongoni mwa viongozi waalikwa waliohudhuria mkutano huo, na hapa anawasilisha salamu zake.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu Mhe. Antony Mavunde akiwasilisha salamu zake kwenye mkutano huo.
Naibu Waziri wa Madini, Mhe, Stanslaus Nyongo akiwasilisha salamu zake. 
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. William Ole Nasha akiwasilisha salamu zake. 
Naibu Waziri OR-TAMISEMI, Mhe. Joseph Kakunda akiwasilisha salamu zake
Viongozi mbalimbali wa chama na serikali wakiwasilisha salamu zao. 

No comments:

Powered by Blogger.