LIVE STREAM ADS

Header Ads

Naibu Waziri Nyongo ambana Mwekezaji kuhusu mpango wa huduma kwa jamii

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Na Greyson Mwase, Dodoma
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo ametoa siku mbili kwa kampuni inayojishughulisha na uchimbaji wa madini ya vito katika Kijiji cha Kwahemu wilayani Chamwino mkoani Dodoma ya Ruvu Gemstone Mining Co. Limited inayomilikiwa na Kimon Dimitri kuwasilisha ofisini kwake ripoti ya utekelezaji wa mpango wa utoaji wa huduma kwa jamii kwa kipindi cha miaka miwili  kabla ya kutoa maamuzi ya serikali.

Naibu Waziri Nyongo aliyasema hayo jana tarehe 06 Oktoba, 2018   alipokuwa akizungumza na wananchi wa  kijiji cha Kwahemu kilichopo Wilayani Chamwino mkoani Dodoma ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku moja  katika Wilaya ya Chamwino  yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini,  kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini pamoja na wananchi wanaozunguka migodi.

Katika ziara yake Nyongo aliambatana na Mkuu wa Wilaya  ya Chamwino, Vumilia Nyamoga, Mbunge wa Jimbo la  Chinolwa, Joel Makanyaga, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Joshua Nduche, vyombo vya  ulinzi na usalama vya Wilaya pamoja na waandishi wa habari.

Alisema kuwa, haiwezekani kampuni inayoendesha shughuli za uchimbaji wa madini ya vito ya Ruvu Gemstone Mining Co. Limited ikaendesha shughuli zake pasipo kunufaisha wananchi wanaozunguka migodi yake.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali kamwe haitamvumilia mwekezaji wa aina yoyote atakayeendesha shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini kwa kukiuka  Sheria Mpya ya Madini  yenye kipengele kinachowataka wawekezaji kuchangia katika uboreshaji wa huduma za jamii ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vituo vya afya, miundombinu ya barabara na shule.

“Serikali kupitia Wizara ya Madini imejipanga katika kuhakikisha watanzania wote wananufaika na uwepo wa rasilimali za madini kupitia kodi, tozo mbalimbali pamoja na mpango wa utoaji wa huduma za jamii,” alisema Naibu Waziri Nyongo.

Alisisitiza kuwa, ni lazima nakala za ripoti zisambazwe kwa Mwenyekiti wa Kijiji, Diwani na Mbunge ili kubaini  ukweli wa madai ya mwekezaji kuwa amekuwa akichangia katika huduma za jamii tangu alipoanza kuchimba madini ya vito mwaka 1986.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Nyongo alimtaka mwekezaji  kuhakikisha anadumisha mahusiano na jamii inayozunguka mgodi  ili kuepusha migogoro inayotokea mara kwa mara.

Awali wakiwasilisha kero kwa Naibu Waziri Nyongo wananchi wa kijiji hicho walimweleza kuwa tangu kuanzishwa kwa mgodi husika hawajaona manufaa ya aina yoyote zaidi ya kunyanyaswa kwa kunyang’anywa ardhi, kupigwa na wakati mwingine kufungwa jela.

Akiwasilisha kero kwa niaba ya wananchi hao, Daudi Kiloka ambaye ni mkazi wa kijiji cha Kwahemu alisema kuwa awali walikuwa na shamba kubwa lenye ukubwa wa takribani heka 500  chini ya Umoja wa Bega kwa Bega wa kijiji hicho lakini baadaye shamba hilo lilikuja kutwaliwa na mwekezaji huyo.

Aliendelea kusema kuwa, wananchi wamekuwa wakikosa huduma muhimu ikiwa ni pamoja na shule, maji na vituo vya afya  hali inayolazimu wananchi wengi kutumia muda mwingi kusafiri umbali mrefu kwa ajili ya kufuata huduma.

No comments:

Powered by Blogger.