LIVE STREAM ADS

Header Ads

Madaktari bingwa kutoka China wawasili nchini

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com


Mkurugenzi Taasisi ya Mifupa MOI iliyopo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili Jijini Dar es salaam, Dkt. Respicious Boniface akizungumza kuhusu hali ya utaoji huduma wa taasisi hiyo katika hafla ya kupokea jopo la madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Peking kutoka nchini China.

Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Prof. Lawrence Mseru akichangia mada katika hafla ya kupokea madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Peking cha China.

Profesa Yuanli Zhao kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Peking cha China akiwasilisha mada kuhusu Hospitali hiyo inavyotoa huduma za kibingwa za hali ya juu kwa kutumia teknolojia ya kisasa.

Daktari bingwa wa upasuaji wa ubongo, mgongo na mishipa ya fahamu kutoka taasisi ya MOI Dkt. Nicephorus Rutabansibwa akitoa taarifa ya hali ya huduma za matibabu na upasuaji wa ubongo, mgongo na mishipa ya fahamu katika taasisi hiyo.

Sehemu ya wajumbe wa Menejimenti wa Taasisi ya MOI na MNH wakifuatilia jambo katika hafla ya kuwapokea madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Peking cha China.

Mkuu wa Kitengo cha dharura cha Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Juma Mfinanga akiwasilisha mada katika hafla ya kupokea madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Peking cha China

Bwana Nathan Chimoto akitoa taarifa ya hali ya utoaji huduma katika kitengo cha uangalizi maalum cha MOI katika hafla ya kupokea madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Chuo Kikuu cha Peking cha China.
Na Khamis Mussa, Dar
Madaktari bingwa watatu wa upasuaji wa ubongo, mgongo na mishipa ya Ffahamu (Neurosurgeon) kutoka hospitali ya kimataifa ya Chuo Kikuu cha Peking cha nchini China, wamewasili katika taasisi ya MOI ambapo wataendesha mafunzo ya nadharia siku ya leo na kuendesha kambi ya upasuaji siku ya jumatatu tarehe 25/02/2019.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya MOI, Profesa Charles Mkonyi amesema ujio wa madaktari bingwa hawa umewezekana kufuatia maagizo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. John Pombe Magufuli ya kuhakikisha Hospitali ya MOI na Chuo kikuu MUHAS zinaingia mkataba wa ushirikinao na Hospitali ya Peking jambo ambalo limetekelezwa chini ya Wizara ya Afya ,Maendeleo ya Jamii, Jinsia ,Wazee na Watoto inayoongozwa na Mh. Ummy Mwalimu.

Katika utekelezaji huo, taasisi ya MOI na Peking zimeingia mkataba wa ushirikiano katika maeneo ya tiba, utafiti na mafunzo. Mkataba huo ulisainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa MOI Dkt. Respicious Boniface pamoja na Rais wa Peking Profesa. Hongxia Yu ambapo MOI inanufaika katika kuboresha huduma za kibingwa za daraja la juu (Super specialised services) katika maeneo ya upasuaji wa Mifupa, Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu.

Mkurugenzi Mtendaji wa MOI, Dkt. Respicious Boniface amesema ujio wao utasaidia kuwajengea uwezo wataalamu wa ndani kwa kuwapa mbinu mpya za upasuaji na hivyo watanzania kupata huduma bora na za kibingwa za Mifupa, Ubongo,Mgongo na Mishipa ya Fahamu bila kwenda nje ya nchi.

"Tunamshukuru sana Mh Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutuletea wataalamu hawa, Hospitali yetu ya MOI itanufaika sana kwani wenzetu hawa wana uzoefu mkubwa katika utoaji wa huduma hususani hizi ambazo tunatoa hapa MOI, binafsi nilifanikiwa kuiona hospitali yao kwakweli ni ya viwango vya kimatifa, sisi pia tunatamani kufikia viwango hivyo". Alisema Dkt. Boniface.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Profesa Lawrence Mseru amesema ushirikiano huu utakuwa wenye manufaa makubwa kwa Watanzania kwani Hospitali ya Peking ni bora kutokana na uzoefu wa wataalamu wake pamoja na miundo mbinu ya kisasa hivyo kufanya huduma zake kuwa bora.

“Mwaka jana mimi pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa MOI tulipata fursa ya kutembelea hospitali hii ya Peking, kwa kweli ni Hospitali kubwa ,nzuri na yenye huduma bora sana, naamini kupitia ushirikiano huu watashirikiana nasi kuboresha huduma hapa nchini” alisema Prof. Museru.

No comments:

Powered by Blogger.