LIVE STREAM ADS

Header Ads

Zaidi ya wanafunzi 300 wapachikwa mimba wilayani Magu

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
 Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Wanafunzi wa kike 301 katika Wilaya Magu mkoani Mwanza wameelezwa kukatisha masomo katika kipindi cha mwaka 2016/19, baada ya kupata ujauzito huku zaidi ya asilimia 90 wakitoka katika Shule za Sekondari.

Mkuu wa Polisi Dawati la Jinsia na Watoto wilayani Magu, Amani Migoha alitoa takwimu hizo Agosti 13, 2019, kwenye kikao cha utoaji elimu ya kupambana na ukatili wa kijinsia katika jamii kwa madiwani, watendaji na viongozi mbalimbali wa Halmashauri ya Wilaya Magu.

Migoha alisema mwaka 2016 kesi za mimba/ ndoa za utotoni zilizoripotiwa polisi zilikuwa 71, 2017 kesi 67, 2018 kesi 106 na mwaka huu tayari kesi 57 zimeripotiwa na kwamba changamoto ya utoaji ushahidi imekuwa ikikwamisha kesi hizo kupata mafanikio mahakamani.

Akifungua kikao hicho, Mkuu wa Wilaya Magu, Dkt. Philemon Sengati aliwataka viongozi wilayani humo kila mmoja kutimiza wajibu wake ipasavyo ikiwemo kutoa elimu hadi ngazi ya jamii ili kuhakikisha matukio ya aina hiyo yanatokomezwa.

Baadhi ya washiriki wa kikao hicho walitoa baadhi ya sababu walizoshauri zitafutiwe ufumbuzi ili kupambana na hali hiyo kuwa ni pamoja na ujenzo wa mabweni hususani kwa wanafunzi wa kike ili kuwaepusha na vishawishi wanapotembea umbali mrefu kwenda shule na kukemea tabia ya baadhi ya wazazi na walezi kuwashawishi watoto wao kuolewa ili wapate mahari.

Kikao hicho ni mwanzo wa utayari kwa viongozi na watendaji mbalimbali wilayani Magu katika kuelekea kwenye utekelezaji kwa vitendo kampeni/ mpango mkakati wa kitaifa wa kupambana na aina zote za ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto (MTAKUWWA) kwa kushirikiana na shirika la kutetea haki za wanawake na wasichana (KIVULINI) wilayani humo.
 Mkuu wa Wilaya Magu, Dkt. Philemon Sengati akizungumza kwenye kikao hicho.
 Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Magu, Hilal Elisha akichangia mada kwenye kikao hicho.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la KIVULINI, Yassin Ally akisisitiza jambo kwenye kikao hicho.
 Baadhi ya viongozi na watendaji waliohudhuria kikao hicho.
 Viongozi na wadau mbalimbali waliohudhuria kikao hicho.
 Wadau wakifuatilia kikao hicho.
Tazama BMG Online TV hapa chini

No comments:

Powered by Blogger.