LIVE STREAM ADS

Header Ads

Wasaidizi wa Kisheria wanolewa "elimu ilete tija katika jamii"

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Kahama, Evodia Kyaruzi akizungumza na wahitimu wa mafunzo ya awali ya Sheria (Wasaidizi wa Kisheria) mkoani Shinyanga.
Baadhi ya wahitimu wa mafunzo hayo.
Baadhi ya wahitimu wa mafunzo hayo.
Mkurugenzi wa Shirika la PACESHI, Perpetua Magoke akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo.
 
Meneja Mradi wa kuimarisha upatikanaji wa Haki kwa wote mjini na Vijijini unaotekelezwa na Shirika la PACESHI, John Shija akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya awali ya sheria kwa wasaidizi wa kisheria kutoka Halmashauri sita za Mkoa wa Shinyanga.
Baadhi ya wahitimu wa mafunzo hayo wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali.
Viongozi wakuu wa Shirika la PACESHI wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Kahama, Evodia Kyaruzi (wa pili kushoto).

Na Salvatory Ntandu, Malunde 1 Blog 
Wahitimu 80 wa mafunzo ya awali ya sheria kutoka Halmashauri sita za Mkoa wa Shinyanga, wametakiwa kutojihusisha na vitendo vya rushwa wanapotoa huduma kwa wananchi katika maeneo wanayoishi ili kutokomeza vitendo vya jinai katika jamii.

Kauli hiyo ilitolewa Desemba 16, 2019 na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Kahama, Evodia Kyaruzi wakati akifunga mafunzo ya siku 15 ya wasaidizi wa kisheria yaliyotolewa na shirika lisilo la kiserikali la Paralegal Aid Center Shinyanga (PACESHI) yaliyofanyika mjini Kahama. 

"Toeni huduma za kisheria kwa wazee wasiojiweza, watoto na akina mama wakiwemo wajane ambao haki zao zinaonekana kupokwa na watu wengine ili waweze kupata masaada zaidi kutoka vyombo vya sheria kama vile Mahakama" alisema Kyaruzi. 

Alisema kwenye jamii kuna matukio mengi yanajitokeza kama vile ubakaji kwa watoto,vipigo vya akina mama, migogoro ya Mirathi,na ndoa za watoto za watoto chini ya miaka 18 hivyo ni budi kuhakikisha wanaisadia jamii kuondokana na jinai hizi kutokana mafunzo ya sheria mbalimbali walizofundishwa. 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa shirika la PACESHI, Perpetua Magoke alisema endapo wasaidizi hao wa kisheria wakifanya kazi kwa weledi katika jamii wanazotoka itasaidia kupunguza matukio ya jinai ambayo yanajitokeza mara kwa mara katika mkoa wa Shinyanga. 

"Mmefundishwa sheria mbalimbali hakikisheni elimu mlioipata inaleta matokeo chanya na tija katika jamii zenu kwa kuyasaidia makundi ya watu waliosahaulika katika jamii kama vile wazee na walemavu" alisema Magoke. 

Kwa upande wake Meneja Mradi wa kuimarisha upatikanaji wa Haki kwa wote mjini na Vijijini kutoka shirika la PACESHI, John Shija alisema ili kukidhi mahitaji ya jamii kupata msaada wa kisheria PACESHI imeamua kutoa mafunzo hayo kwa wasaidizi wa kisheria 80 kutoka halmashauri za Msalala, Kishapu, Kahama Mji, Manispaa ya Shinyanga, Ushetu na Halmashauri ya Shinyanga. 

"Tumewafundisha sheria mama ya msaada wa kisheria (Legal Aid Act No 1/2017)ili watambue mbinu mbalimbali za kuwasidia wahitaji ili kupata msaada stahiki wa kisheria" alisema Shija. 

Esta Enock kutoka Halmashauri ya Msalala na Sita Said Mahonja kutoka Manispaa ya Shinyanga walisema mafunzo hayo yamekuwa msaada mkubwa kwao kwani awali walikuwa hawana uelewa kuhusiana na sheria ambapo kwa sasa wataweza kuwahudumia wananchi wengi kwa haraka sana. 

Mafunzo hayo ya siku 15 yalianza mjini Kahama Disemba 02, 2019 na kuhitimishwa Disemba 16, 2019.

No comments:

Powered by Blogger.