LIVE STREAM ADS

Header Ads

Ibada ya kwanza ya Msikiti mpya wa BAKWATA yafanyika 'Dkt. Bashiru ahusishwa'

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Na Baltazar Mashaka, Mwanza
Waumini wa Dini ya Kiislamu pamoja na wadau wengine jijini Mwanza wamehimizwa kuendelea kuchangia na kukamilisha ujenzi wa Msikiti mpya wa Ijumaa wa Abubakar Zuberi Mbwana (Mutfi wa Tanzania), unaomilikiwa na Baraza Kuu la Waislamu (BAKWATA) Mkoa Mwanza.

Rai hiyo ilitolewa Mei 15, 2020 na Sheikhe wa Mkoa wa Mwanza, Alhaji Hasani Kabeke wakati akizungumza kwenye ibada ya kwanza ya Msikiti huo na kuongeza kwamba msikiti huo umeanza kutumiwa kwa ibada na waumini wa dini ya Kiislamu wakati huu wa mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhani huku ufunguzi rasmi ukisubiri kupungua kwa maambukizi ya ugonjwa wa Covid-19 unaosababishwa na kirusi cha Corona.

Pia alitumia fursa hiyo kuwahamasisha waumini wa dini hiyo misikitini na kwenye jamii kujilinda na maambukizi y ugonjwa wa Corona (Covid-19) kuhakikisha wanavaa barakoa,wanatumia vyakula bora (milo iliyokamilika) na matunda yenye vitamini C ili kujiweka vizuri kiafya.

Alisema uamuzi wa kuanza kutumika kwa msikiti huo Mkuu wa Bakwata mkoani hapa kwa ibada umefanyika ili kuwaepusha baadhi ya waumini waliochangia sadaka zao kuujenga wasikose fadhila za mwezi Mtukufu wa Ramdhani licha kuwa haujakamilika bado na kuwaomba wenye uwezo waendelee kuchangia ili kukamilisha ujenzi huo.

“Leo tumeanza kuswali 13 ya Ijumaa ya Ramadhani katika Msikiti Mkuu wa Baraza hilo japo haujakamilika.Tumefanya hivi ili kuwafanya baadhi ya waumini waliotoa sadaka zao kwa ajili ya ujenzi ili wasikose fadhila za mwezi huu na tunashukuru Mwenyezi Mungu mahudhurio yalikuwa makubwa,”alisema Sheikhe Kabeke.

Aidha Sheikhe huyo wa Mkoa wa Mwanza Pia alimshukuru Katibu Mkuu wa CCM Dk. Bashiru Ally kwa mchango wake wa saruji mifuko 100 akiwemo mfanyabiashara mmoja ambaye hakumtaja kwa michango hiyo iliyowezesha kufanyika kwa ujenzi wa nyumba hiyo ya ibada.

“Mtu mwenye kutoa ama kujenga nyumba, hatoi kwa utashi wake bali anatoa kwa imani halisi ya dini yake, nitumie fursa hii kumshukuru Dk. Bashiru Ally (Katibu Mkuu wa CCM) aliyechangia mifuko 100 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa msikiti huu mwaka jana lakini pia wahisani wengine waliojitoa kuchangia hadi tulipofikia kuezeka na msikiti huu ni wa kihistoria,”alisema Sheikhe Kabeke.

Katika hotuba yake ya swala ya Ijumaa Sheikhe huyo wa mkoa, alielezea umuhimu wa kumi la 13 la Ramadhani, ambalo limegawanyika katika mafungu matatu, moja rehema, pili msamaha na la tatu ni kukombolewa na moto kwa kufanya ibada, kusaidia wajane na yatima pamoja na ubora wa mtu anayetoa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za ibada.

Alifafanua kuwa licha ya Bakwata kuwa na misikiti mingi haikuwa na msikiti wake mkuu badala iliteua msikiti mkuu wa kuendeshea ibada ya swala ya siku ya Ijumaa na si kwamba anawabeza waliotangulia la hasha na kutoa wito kwa wenye uwezo waendelee kuchangia waufanye ukamilike, uwe na hadhi yake.

Aliwasitiza waumini wa dini ya kiislamu kuacha kubeza maelekezo ya kujikinga kwenye mapambano dhidi ya ugonjwa wa Corona (Covid-19) badala yake wazingatie iwe misikitini na kwenye jamii kujilinda na kuhakikisha wanavaa barakoa,wanakula milo iliyokamilika na matunda ya kujenga mwili.

No comments:

Powered by Blogger.