LIVE STREAM ADS

Header Ads

TAMKO LA WAANDISHI WAANDAMIZI KUHUSU UCHAGUZI MKUU TANZANIA

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Tamko la Waandishi Waandamizi wa Habari wa Mwanza kuhusu Uchaguzi Mkuu.
Ndugu waandishi wa habari.

Kama mtakumbuka Oktoba 28, mwaka huu, nchi yetu ilifanya Uchaguzi Mkuu kwa nafasi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wa Zanzibar, Wabunge, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar na madiwani.

Kwa bahati nzuri uchaguzi huo muhimu kwa nchi yetu, ulifanyika kwa amani, uhuru na haki na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) iliwatangaza washindi katika ngazi zote hizo nilizozitaja.

Tukiwa waandishi wa habari waandamizi katika nchi hii ambao pia ni wadau muhimu katika suala hili la uchaguzi, tunapenda kumpongeza Rais Mteule John Joseph Pombe Magufuli, ambaye pia alikuwa mgombea urais kupitia CCM, na serikali yake kwa kusimamia suala la amani, haki na uhuru mpaka uchaguzi ulipomalizika.

Ni jambo muhimu sana kwa ustawi wa nchi yetu pale uchaguzi unapofanyika na kumalizika salama. Huu ni ushindi na kielelezo bora kwa nchi yetu mbele ya jumuiya za kikanda na kimataifa.

Sisi kama waandishi wa habari, tunatumia nafasi hii kuwapongeza wagombea wote, lakini kwa kipekee washindi wa ngazi zote walizogombea.

Waandishi wa habari pamoja na majukumu yetu ya kuhabarisha jamii, lakini pia tuna wajibu wa kusema jambo pale tunapoona ustawi wa nchi yetu umeendelea kuimariki chini ya uongozi wa Rais Magufuli.

Tunatoa wito kwa wadau wote kushirikiana na kuhakikisha tunabaki wamoja baada ya kumalizika Uchaguzi Mkuu, na kama alivyosema Rais mteule Magufuli kwamba sasa ni muda wa kuchapa kazi.

Kwa hapa mkoani Mwanza tunapofanyia mkutano huu, tunapongeza pia usimamizi wa usalama na amani kupitia kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Muliro Jumanne Muliro katika kipindi chote cha uchaguzi.

Kazi iliyo.mbele yetu hivi sasa kama waandishi wa habari ni kumuunga mkono Rais Magufuli ili aendelee kuwaletea wananchi maendeleo ya kweli.

Tunajua Rais amekuwa na sisi vizuri kwa miaka mitano na tuna imani ataendelea kuwa hivyo katika miaka mingine mitano atakayowatumikia Watanzania.

Tumeshuhudia maendeleo makubwa katika sekta mbalimbali katika miaka mitano iliyopita na tuna imani Rais Magufuli ataendelea kuwatumikia vyema Watanzania wote.

Kikubwa sisi waandishi wa habari tuhakikishe, tunamuunga mkono kupitia kalamu zetu, kwa kuwaunganisha wananchi wa vyama vyote na jamii kwa ujumla badala ya kuwa chanzo cha kuleta mfarakano.

Asanteni
Richard Makore
Mwandishi Mwandamizi 
Mwanza
03.11.2020
MWISHO.

No comments:

Powered by Blogger.