LIVE STREAM ADS

Header Ads

Maombi ya kuliombea Taifa lipate mvua yapamba moto

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Online Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Mkuu wa Wilaya ya Same Edward Mpogolo akizungumza katika mkutano wa maombi maalumu wa kuliombea Taifa lipate mvua uliofanyika wilayani humo.

Mkutano ukiendelea.
Mkutano ukiendelea.
Viongozi wa Dini wakiwa kwenye mkutano huo.
Mkuu wa Wilaya ya Same Edward Mpogolo akisisitiza jambo kwenye mkutano huo.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Same Isaya Mngulu, akizungumza wakati wa maombi hayo.
Askofu Mstaafu Jimbo Katoliki la Same Jacob Koda akizungumza kwenye mkutano huo.
Mkutano ukiendelea.
Mkuu wa Wilaya ya Same Edward Mpogolo (katikati waliokaa) akiwa na viongozi wa Dini na Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kufanya maombi maalumu ya kuombea nchi ipate mvua.

Na Mwandishi Wetu, Same
Mkuu wa Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, Edward Mpogolo ameongoza maombi maalumu ya kuiombea nchi ipate mvua ili kunusuru maisha ya watu na wanyama.

Maombi hayo muhimu yaliwahusisha, viongozi wa dini, wazee pamoja na wananchi.

Kati ya maeneo ambayo yanatajwa kuathirika zaidi na mabadiliko ya tabia ya nchi na kukosekana kwa mvua ni pamoja na wilaya hiyo ambayo wakazi wake ni wafugaji na wakulima.

Akizungumza jana wakati wa ufunguzi wa mkutano wa maombi hayo, Mkuu wa Wilaya hiyo, Edward Mpogolo alisema changamoto kubwa iliyopo kwa sasa ni ukame unaoyakabili maeneo mbalimbali ya tambarare ndani ya wilaya hiyo huku wahanga wakubwa wakiwa ni wafugaji, wakulima pamoja na wanyama.

Mpogolo alisema Serikali wilayani hapo imeunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuwataka viongozi mbalimbali kuungana na viongozi wa dini na wa kimila katika kuliombea Taifa ili Mungu aweze kushusha mvua ya wastani kwa mahitaji ya wananchi ikiwa ni pamoja na kutunza vyanzo vya maji na kumhimiza utunzaji wa mazingira.

"Nimewaita wazee wangu pamoja na viongozi wa dini ili tuweze kujadili kwa pamoja nini tunaweza kufanya na kuokoa maisha ya wananchi wetu pamoja na mifugo, "alisema Mpogolo.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazee Wilaya ya Same (JUWASA), Deoglas Msangi alisema mabadiliko ya tabia ya nchi yanayojitokeza sehemu mbalimbali hapa nchini yamesababishwa na uhalibifu wa mazingira ambao unafanyika katika maeneo mengi.

Msangi alisema kwa sasa kumekuwapo na uvunaji miti kiholela katika maeneo mengi kitu ambacho kinasababisha maeneo hayo kuwa makame na kukausha vyanzo vya maji.

"Zamani kulikuwa na misitu mingi ya asili ambayo wazee wetu waliitunza kwa lengo la kutunza mazingira sambamba na utunzaji wa vyanzo vya maji na mafanikio yake yalionekana kwa jamii lakini hivi sasa misitu mingi haipo na ukame umezidi hivyo inatupasa tubadilike," alisema Msangi.

Baadhi ya viongozi wa dini wakiongozwa na Askofu Mstaafu Jimbo Katoliki la Same Jacob Koda, Askofu Msaidizi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Pare, Ibrahim Ndekia, Askofu Kanisa la TAG Paulo Ponda, Sheikh Mkuu wa Wilaya ya Same, Idd Juma Ally wamesema ili taifa lifunguliwe ni lazima kufanyika Sala ya Toba kwa wananchi kwani kwa kiasi kikubwa jamii imemkosea Mungu.

Viongozi hao walijumuika pamoja na Serikali na waliongoza kuliombea Taifa Ili Mungu aweze kushusha mvua ya wastani kwa mahitaji ya Wananchi, wakulima na wafugaji huku wazee hao wakiiomba Serikali iwajengee mabwawa yatakayotumika kuvuna maji ya mvua yatakayosaidia wafugaji na wakulima kipindi cha ukame.

No comments:

Powered by Blogger.