LIVE STREAM ADS

Header Ads

RUWASA Kahama yajivunia mafanikio utekelezaji miradi ya maji

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Kahama Thomas Myonga akikabidhi vifaa vya ufundi kwa baadhi ya viongozi wa vyombo vya watumia maji (CBWOSO)
Kaimu Meneja wa Ruwasa Kahama Mhandisi Pascal Mnyeti akizungumza na baadhi ya viongozi wa vyombo vya watumia maji hawapo pichani
Katibu tawala wa wilaya ya Kahama Timothy Ndanya ambaye ni Mgeni rasmi katika mkutano wa vyombo vya watumia maji wilaya ya kahama kushoto ni mhandisi Cyprian Ndabavunye
Mwakilishi wa meneja wa Ruwasa mkoa wa Shinyanga mhandisi Cyprian Ndabavunye akisikiliza hoja kwenye mkutano mkuu
Mhandisi Luchangaya Paul mwakilishi wa Kuwasa akichangia mada kwenye mkutano wa vyombo vya watumia maji


Na Mwandishi wetu, Kahama
Zaidi ya wakazi laki tano wanaoishi vijijijini wilayani Kahama mkoani Shinyanga wameondokana tatizo la kuchangia maji na mifugo baada ya serikali kupitia Wakala wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kujenga miradi ya maji.

Hayo yamebainishwa leo Jumatano Mei 24,2024 kwenye mkutano wa vyombo vya watumia maji wilaya ya Kahama, na Kaimu Meneja wa Ruwasa wilaya ya Kahama Mhandisi Paschal Mnyeti wakati akisoma taarifa ya hali ya upatikanaji wa huduma za maji vijijini na hatua za utekelezaji wa miradi inayoendelea kutekelezwa.

Amesema kuwa hali ya upatikanaji wa huduma za maji safi na salama katika wilaya ya Kahama kwa sasa ni asilimia 68 ambapo kwa kipindi cha Julai 2022 hadi sasa RUWASA imetekeleza miradi ya maji mbalimbali katika halmashauri za Msalala,Ushetu na Manispaa ya Kahama.

“Tumetekeleza miradi ya Maji 14 yenye thamani ya Shilingi bilioni 17.1 ambapo katika Halmashauri ya Msalala miradi Saba,Ushetu miradi minne na Manispaa ya Kahama miradi mitatu na kati ya miradi hiyo mitano imetumia shilingi bilioni tatu imekamilika na inatoa huduma kwa wananchi,”amesema Mnyeti.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Meneja wa RUWASA mkoa wa Shinyanga Mhandisi Cyprian Ndabavunye amewataka viongozi wa vyombo vya watumia Maji (CBWOSO)kuhakikisha wailinda miradi hiyo ili iweze kuleta tija kwa wananchi.

“Boresheni huduma kwa wananchi vijijini ikiwa ni pamoja na kuwasongezea mtandao wa maji kwenye makazi yao sambamba na kutatua changamoto za kiufundi zinazoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji wa miradi hiyo,”amesema Ndabavunye.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kahama Thomas Myonga amesisitiza juu ya ujenzi wa mradi wa maji ya ziwa Victoria ambao umeanza kutekelezwa kutoka Kahama kwenda katika halmashauri ya Ushetu ili kuwaondolea adha wananchi kufuata huduma za maji mbali na makazi yao.

“Taarifa yenu inaonesha usanifu wa mradi huu umekamilika nawaomba muongeze juhudi ili tuwaondolee wananchi wa Ushetu adha ya kutafuta umbali mrefu baada ya serikali kutenga fedha kupekeleka maji katika halmashauri hii,”amesema Myonga.

Awali akifungua mkutano huo katibu Tawala wa wilaya ya Kahama Timothy Ndanya ambaye alikuwa ni mgeni rasmi ameagiza Ruwasa kuwasimamia wakandarasi wanaotekeleza miradi ya maji vijiji ili ikamilike kwa wakati na watakoshindwa hatua zichukuliwe.

“Ofisi yangu inataarifa za baadhi ya wakandarasi kuchelewesha miradi ya Maji,wapeni salamu hatutasita kusitisha mikataba yao sisi tunachotaka wananchi wapate maji kwa wakati kama mikataba yao inavyoelekeza,”amesema Ndanya.

No comments:

Powered by Blogger.