LIVE STREAM ADS

Header Ads

Katibu Mkuu CCK ataka sakata la bandari lifikie tamati

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Katibu Mkuu wa CCK, Renatus Muabh.


Na Emmanuel Thobias
Chama Cha Kijamii (CCK) kimetahadharisha kuwa malumbano yanayoendelea kuhusu uwekezaji wa bandari ya Dar es Salaam hayana afya na yanaligawa taifa na hivyo kimeitaka serikali, Chama Cha Mapinduzi (CCM),vyama vya siasa vya upinzani na wadau wengine wazalendo kufikia muafaka wa kuruhusu maoni ya wananchi yafikie mwisho.

Katibu Mkuu wa CCK, Renatus Muabhi katika taarifa yake aliyoisambaza kwa vyombo vya habari leo (Julai 18, 2023),amesema ili kufikia mwafaka wa suala hili kuna haja ya kuandaa mdahalo wa kitaifa ili kutathimini msimamo wa serikali na maoni ya wananchi.

Muabhi alisema njia nyingine ya kufikia tamati suala hili ni kuunda tume huru ya wadau itakayoshirikisha wajumbe kutoka makundi tofauti yenye mawazo huru, kukusanya maoni na kutathimini msimamo wa wananchi, jambo ambalo litaleta muafaka na maridhiano kwa makundi yote yanayokinzana.

"Kikatiba mamlaka ya nchi yapo chini ya wananchi, tutafute na tuelewe maoni ya wananchi yanataka nini na hofu yao ni nini, hofu na mashaka yao vikiondolewa kwa kuridhiwa, tuanze utekelezaji wa uwekezaji kwa kuwa hofu na mashaka vitakuwa vimetibika kwa mamlaka ya wananchi wenyewe," alisema.

Muabhi aliongeza kuwa tusiruhusu kelele uchwara za wachache wenye hila zao binafsi, kutaka kuburuza umma kwa tamaa zao za mali jambo ambalo halitasaidia kumaliza mvutano huo.

" Wananchi wakionesha mashaka na kutoridhia, tuachane mara moja na mkataba huu pamoja na hatua zake zote zinazopaswa kufuata ili kuepusha serikali na chama tawala cha ccm, kutumia nguvu ya dola kushinikiza jambo kwa wananchi," alisema Muabhi.

Alisema viongozi lazima watambue kuwa Serikali iliyopo madarakani ni ya watu, iliwekwa na watu kwa ajili ya watu na wanaipenda hivyo wanayomamlaka kisheria kuikosoa bila kutishwa.

"Niwakati wa maridhiano, tukiri umoja wetu umetikiswa, imani ya wananchi kwa serikali yao imetoweka, michuano hii ya hoja inakoleza maswali kwa wananchi wasiojua mambo ya siasa na mikataba, ni wakati wa maridiano," alisema.

No comments:

Powered by Blogger.