LIVE STREAM ADS

Header Ads

Tabora wajipanga kupambana na Malaria

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Kaimu Meneja Bohari ya Dawa (MSD) Mkoa wa Tabora Adonizedeck Tefurukwa, akizungumzia kuhusu hali ya ugonjwa wa malaria katika Mkoa wa Tabora katika kambi iliyowekwa na MSD kwa ajili ya kugawa vyandarua mkoani humo.
***

Mkoa wa Tabora umetajwa kuwa wa kwanza kitaifa kuwa na kiwango kikubwa cha maambukizi ya ugonjwa wa Malaria hali inayotokana na imani potofu ya matumizi ya vyandarua vyenye dawa kuwa vinapunguza nguvu za kiume.

Akizungumza Septemba 25, 2023 Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Luis Bura amesema hali ya ugonjwa wa Malaria ni mbaya na mkoa huo ndio unaongoza kwa maambukizi ya ugonjwa huo.

Amesema takwimu zinaonyesha kiwango cha maambukizi ya malaria kimeongezeka kutoka asilimia 11.7 mwaka 2016/2017 hadi asilimia 23.4 mwaka 2022 wakati kiwango cha maambukizi ya malaria kitaifa ni asilimia 8.1.

Hivyo kutokana na hali hiyo Serikali kupitia Bohari ya Dawa (MSD) imetia kambi mkoani humo na kusambaza vyandarua vyenye dawa.

“Tafiti zinaonyesha kiwango cha maambukizi ugonjwa wa malaria kwa mwaka 2016/2017 kwa watoro wa umri wa miezi sita hadi miaka 5 ni asilimia 20 na mwaka 2018 yameongezeka kufikia asilimia 23” amesema.

Akizungumzia kiwango cha maambukizi ya ugonjwa huo kitaifa ni asilimia 8.1 hivyo ongezeko hilo ni sawa na asilimia 11.7 hali inayosababisha mkoa huo kuongoza huku akieleza hali hiyo haikubaliki, hivyo ni lazima kuwa na nguvu ya pamoja kwa watendaji na jamii kuhakikisha maambukizi hayo yanapungua.

Amefafanua kuwa makundi ambayo yako hatarini ndio yatanufaika na vyandurua hivyo wakiwemo watoto chini ya miezi tisa na miaka mitano, wajawazito, wanafunzi , wazee wa miaka 60 na watu wanaoishi na VVU.

Ameongeza kuwa kaya zaidi ya 300,000 kati ya kaya 400,000 ambazo zitapewa vyandarua hivyo ambavyo ni zaidi ya milioni 1.8.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa MSD Tabora Adonizedeck Tefurukwa, ameushukuru uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha huduma za afya nchini na kuwahakikishia wananchi wa Tabora kuwa, kila mnufaika wa vyandarua hivyo atafikiwa.

Amesema katika usambazaji huo wamejipanga ipasavyo na wanatimu ya kutosha kufika katika kila maeneo na ili kufanikisha hatua hiyo, wamekodisha maghala mawili ya ziada eneo la Nzega na Igunga.

Wakati huo huo Mganga Mkuu wa Mkoa Dk. Honoratha Rutatinisibwa amesema takwimu hizo zinatokana na mkoa huo wananchi wake kuwa na imani potufu ya matumizi ya vyandarua vyenye dawa kuwa vinapunguza nguvu za kiume.
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tabora Luis Bura akizungumzia ugonjwa huo.
Mganga Mkuu wa Mkoa Dk. Honoratha Rutatinisibwa.
Taarifa ya maambuzi ya ugonjwa wa malaria ikitolewa.
Taarifa ya maambukizi ya ugonjwa wa malaria ikitolewa.

No comments:

Powered by Blogger.