LIVE STREAM ADS

Header Ads

Tume ya Taifa ya UNESCO yatoa mafunzo kwa wanafunzi Shinyanga

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wakifuatilia mafunzo kuhusu madhara ya ndoa za utotoni na ukatili wa kijinsia.
Mshauri Mwelekezi wa Mradi wa Kupinga Ndoa za Utotoni unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Rehema Horera John.
***

Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa mafunzo kuhusu Madhara ya Ndoa za Utotoni na Ukatili wa Kijinsia kwa wanafunzi wa kike kutoka shule za msingi kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga mkoani Shinyanga kwa lengo la kupinga ndoa za utotoni.

Mafunzo hayo ni Programu ya kuandaa mabinti mabalozi wa kupinga Nndoa za utotoni ambayo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi shirikishi wa Tume ya UNESCO wa kupinga ndoa za utotoni, yamefanyika Septemba 05, 2023 katika ukumbi wa Halmashauri ya Shinyanga uliopo Iselamagazi.

Mshauri Mwelekezi wa Mradi wa Kupinga Ndoa za Utotoni unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO kwa ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), Dkt. Rehema Horera John amesema wanafunzi wa kike wa shule za msingi ni miongoni mwa walengwa wa Programu hiyo ambao wanapewa elimu ya uhamasishaji kuhusu madhara ya ndoa za utotoni na masuala ya ukatili kwa ujumla kwa watoto.

“Tumeamua kukutana na wanafunzi wa kike kwa sababu ni waathirika wakubwa ni watoto wa kike hasa wenye umri wa miaka kati ya 8 hadi 18, lakini pia tutaendelea kukutana na makundi mengine ya wanafunzi wakiwemo wa kiume kwani pia wanayo nafasi kubwa ya kuzuia vitendo vya ukatili wa kijinsia lakini pia nao wamekuwa wakikumbana na vitendo vya ukatili ikiwemo ulawiti” ameeleza Dkt. Rehema.
Mshauri Mwelekezi wa Mradi wa Kupinga Ndoa za Utotoni unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Rehema Horera John akitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike.

“Tume ya Taifa ya UNESCO inatekeleza Programu hii katika kata za Lyabusalu, Ilola na Iselamagazi kwa ufadhili ya UNESCO lengo kubwa ni kupinga ndoa za utotoni katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga” amesema Dkt. Rehema.

Dkt. Rehema amewataka wanafunzi wa kike kuepuka kukaa kimya badala yake watoe taarifa endapo watabaini kuwepo kwa dalili za kufanyika kwa ukatili wa kijinsia.

“Ukatili wa kijinsia unazuilika, ndoa za utotoni zinazuilika hivyo ukiona dalili ya ukatili wa kijinsia toa taarifa mapema kwa mtu unayemuamini. Tuzipambanie ndoto zetu, tutimize ndoto zetu” amesema.

“Mwanafunzi epuka vishawishi vyote ambavyo vitakurudisha nyuma, usiwe na mchezo kwenye mambo yanayokurudisha nyuma.Usikubali kuitwa mchumba. Kwepa ndoa za utotoni, kwepa ndoa za kulazimishwa. Epuka kuvaa nguo fupi na nguo za kubana naepuka kujipitisha pitisha kwa wanaume” ameongeza Dkt. Rehema.
Aidha amewasihi wanafunzi kuepuka kutembea usiku, sherehe za usiku, ngoma za usiku kwa sababu shughuli nyingi za usiku zinahatarisha usalama wa mtoto ikiwemo kumuweka katika hatari ya kufanyiwa vitendo vya ukatili.

“Mmomonyoko wa maadili katika jamii, matumizi ya dawa za kulevya na pombe ni miongoni mwa vichocheo vya ukatili wa kijinsia hivyo ni lazima tuviepuke ili watoto wawe salama ingawa umaskini na baadhi ya mila kandamizi zimekuwa zikisababisha vitendo vya ukatili. Jamii inatakiwa iendelee kupewa elimu kuhusu madhara ya vitendo vya ukatili wa kijinsia” ameeleza Dkt. Rehema.
Wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wakiwasilisha kazi ya kikundi.


Kwa upande wao wanafunzi hao wa kike, licha ya kuahidi kuwa mabalozi wazuri wa kuelimisha wanafunzi wenzao pia wameiomba serikali kutunga sheria kali za kuzuia ndoa za utotoni huku wakishauri elimu iendelee kutolewa kwa jamii kuhusu madhara ya ndoa za utotoni na ukatili wa kijinsia.

Wanafunzi hao wamekubaliana kwa pamoja kutokubali kukatishwa masomo ili waolewe, kukataa kuambiwa wafeli mitihani ili waolewe, kuepuka kuguswa miili yao ‘Don’t touch’ na mwanaume au mwanamke bila ridhaa.

Afisa Elimu Maalum Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Irene Kisweka amesema wanafunzi hao waliopatiwa mafunzo wataenda kutoa elimu hiyo kwa wanafunzi wenzao kupitia Klabu za Kupinga ukatili wa kijinsia ili kuhakikisha kuwa shule zote zinapata elimu ya ukatili wa kijinsia.

“Mkawe majasiri, muende mkapeleke elimu hii katika shule zenu, waelimisheni pia watoto waliokatishwa masomo kwa kupewa mimba au kuolewa wakiwa wadogo ili vitendo vya ukatili visiendelee kujitokeza” amesema.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Aboud Khamis amesema ndoa za utotoni bado zipo katika jamii hivyo kuwataka wanafunzi hao kuwa mabalozi wazuri kwa wenzao shuleni na katika jamii ili kuhakikisha ndoa za utotoni zinatokomezwa.

Aidha amewakumbusha wanafunzi kuchukua tahadhari dhidi ya ukatili wa kijinsia kupitia mitandao ya kijamii akiwaka kuepuka msiangalia picha chafu kupitia simu za mkononi ili wasijifunze mambo mabaya.

Naye Afisa Programu Mkuu Sayansi ya Jamii kutoka Tume ya Taifa ya UNESCO, Bi. Uyanjo Lazarus amefafanua kuwa, mafunzo hayo yaliyolenga kuandaa Mabinti kuwa Mabalozi wa Kupinga Ndoa za utotoni yatasaidia kwa kiasi kikubwa kufikisha elimu kwa wanafunzi kuhusu madhara ya ndoa za utotoni.
Na Kadama Malunde, Malunde 1 Blog
Mshauri Mwelekezi wa Mradi wa Kupinga Ndoa za Utotoni unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Rehema Horera John akitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. 
Mshauri Mwelekezi wa Mradi wa Kupinga Ndoa za Utotoni unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Rehema Horera John akitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga
Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Aboud Khamis akizungumza wakati Tume ya Taifa ya UNESCO ikitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.
Afisa Elimu Maalum Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Irene Kisweka akizungumza wakati Tume ya Taifa ya UNESCO ikitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.
Afisa Programu Mkuu Sayansi ya Jamii kutoka Tume ya Taifa ya UNESCO, Uyanjo Lazarus akizungumza wakati Tume ya Taifa ya UNESCO ikitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.
Afisa Programu Mkuu Sayansi ya Jamii kutoka Tume ya Taifa ya UNESCO, Bi. Uyanjo Lazarus akizungumza wakati Tume ya Taifa ya UNESCO ikitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.
Afisa Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Aisha Omary ambaye pia ni Mratibu wa MTAKUWWA halmashauri hiyo akizungumza wakati Tume ya Taifa ya UNESCO ikitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyang
Mkuu wa Divisheni ya Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Joseph Ntomela akizungumza wakati Tume ya Taifa ya UNESCO ikitoa elimu kuhusu madhara ya ndoa za utotoni kwa wanafunzi wa kike kutoka kata za Ilola, Lyabusalu na Iselamagazi halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

No comments:

Powered by Blogger.