LIVE STREAM ADS

Header Ads

AFYA ZA WATUMIAJI MAJI ZIWA VICTORIA HATARINI...HII NI KUTOKANA NA UTIRIRISHAJI WA VINYESI KWENYE MITO INAYOMWAGA MAJI YAKE KATIKA ZIWA HILO.


Usafi ukiendelea
Zaidi ya Kaya 75 Jijini Mwanza zinazouzunguka Mto Mirongo ambao unamwaga Maji yake katika Ziwa Victoria, Zimebainika kutiririsha vinyesi na majitaka ndani ya Mto huo hali inayoongeza kasi ya Uchafuzi wa Mazingira sanjari na kuhatarisha afya ya watumiaji wa Maji ya Ziwa Victoria ikiwemo mimea na viumbe hai waishio Majini.
 
Hayo yalibainishwa jana na baadhi ya wadau wa mazingira kutoka Ofisi za Maji Bonde la Ziwa Victoria, Maafisa wa Afya wa Jiji la Mwanza na Jumuia ya Watumiaji wa Maji na Utunzaji wa Mazingira walipokuwa wakifanya usafi Katika Mto huo ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani ambayo inafikia kilele chake June Tano Mwaka huu. 

Kaimu Afisa wa Maji kutoka Bonde la Ziwa Victoria Godfrey Kajanja alisema kwamba, Ofisi yake na Halmashauri ya Jiji zitakutana kuchukua hatua za kisheria kwa Kaya hizo na watu walio na tabia ya kuchafua maji ya mito ikiwemo Mto Mirongo.

Kajanja alisema kwamba, hali hiyo ikiachwa kuendelea bila kudhibitiwa kutawezesha kuibuka magonjwa ya kuambukiza ikiwa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Mkoani  Mwanza haitachukua hatua za kuongeza kiasi kikubwa cha dawa ya kutibu maji kabla ya kusambazwa kwa watumiaji.

“Lazima sasa tushirikiane kuzitekeleza sheria zilizopo za Mipango miji kwa upande wa Jiji la Mwanza, pamoja na ofisi yetu ya Bonde kutumia sheria ya usimamizi wa rasilimali ya maji Na. 11/2009 na sheria ya usimamizi wa mazingira Na. 24/2004 ambazo zinaoanisha adhabu ya fedha na kifungo kwa watu watakaokaidi na kukutwa na makosa,” alisema.
Kwa upande wake Mhandisi wa Maji toka ofisi za Bonde la Ziwa Victoria Mhandisi Jane John alieleza kwamba, hatua hivyo inatakiwa kukomeshwa mara moja na jamii iliyo kandokando ya maeneo unapipita mto Miringo na maeneo ya vyanzo vya maji ili kusaidia kulinda na tabia ya uchafuzi wa mazingira ikiwemo udhibiti jambo ambalo litaepusha uharibifu na uchafuzi.


“Tumeshuhudia mabomba ya vinyesi na maji machafu yakimwaga mtoni wakati tukifanya usafi wa pamoja kwenye mto Mirongo na wadau mbalimbali walioko kwenye maadhimisho ya siku ya mazingira kitaifa hili ni jambo ambalo linahitaji hatua za haraka kulikomesha na kuwachukulia hatua wanaofanya uchafuzi huu,”alisisitiza.
Naye Mwenyekiti wa NGO ya Jumuiya ya watumiaji maji na mazingira Adam Shija ya Kata ya Mbugani Wilayani Nyamagana mkoani hapa alisema kwamba, tumekuwa na changamoto kubwa wakati wa usafishaji wa mto huo na wamebaini kuwepo kwa baadhi ya Kaya 75 ambazo zimekuwa zikitirilisha uchafu wa vinyesi na majimachafu ndani ya mabomba yaliyoelekezwa mtoni humo.

Shija alifafanua walipotembelea kandokando ya mto huo kwenye maeneo ya unapoanzia na kupitia kasha kumwaga maji ziwani Victoria katika Kata za Nyakato walibaini kaya 16, Mahina kaya 8, Mbugani kaya 24, Mirongo kaya 17, Nyamagana kaya 6 na Pamba kaya 4 na tayari orodha hiyo imetokana na ukaguzi wa Jumuiya hiyo hivi karibuni.

“Wito wangu kwa Serikali na Idara zenye jukumu la kusimamia rasilimali ya maji na mito, mabwawa na ziwa Victoria kutekeleza sheria kwa vitendo ili kukomesha tabia hii ya uchafuzi wa maji na uharibifu wa mazingira unaofanywa kwa makusudi na baadhi ya wananchi bila kujali kama husababisha madhala kwa watumiaji wa maji na kuhatarisha uhai wa viumbe hai majini”.

Shughuli mbalimbali zinaendelea wiki hii ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya Mazingira duniani ambapo Kitaifa maadhimisho hayo yanafanyika katika uwanja wa Furahisha Mkoani Mwanza.Rais Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho hayo ambapo atashiriki katika zoezi la kuwakabidhi tuzo washindi mbalimbali ambao wameshiriki vyema katika shughuli za utunzaji wa mazingira.
Na:Gsengo Blog

No comments:

Powered by Blogger.