WANANCHI WA WILAYA UKEREWE MKOANI MWANZA WAILILIA CCM, WASEMA KAMA NI ADHABU IMETOSHA.
Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji Wazazi Mkoa wa Mwanza kupitia Chama cha Mapinduzi CCM Alfred Wambura, amebainisha kwamba CCM imejipanga vyema katika kuhakikisha inapata ushindi mnono katika chaguzi zijazo za Serikali za Mitaa sanjari na Uchaguzi Mkuu ujao wa mwaka 2015.
Mjumbe huo alitoa kauli hiyo hivi karibuni Mkoani Mwanza wakati
akizungumza na Radio Metro juu ya Mstakabali wa Chama cha Mapinduzi CCM,
sambamba na uteuzi wake uliofanyika mwezi uliopita ambapo aliteuliwa kuwa
Kamanda wa Vijana wa CCM katika Kata ya Nyakato Wilayani Ilemela.
Alibainisha kwamba hivi sasa CCM ni kama imeamka kutoka usingizini
baada ya kujisahau na kujikuta inapoteza baadhi ya majimbo katika uchaguzi
uliopita ambapo baadhi ya majimbo yalichukuliwa na vyama vingine vya upinzani.
“Yaani ninachokuhakikishia ni hivi CCM tumeamka, Tumeamka unajua mimi
huwa natumia msemo kwamba hawa wapinzani ni kama jogoo ndani ya nyumba, mara
nyingi jogoo ndani ya nyumba linapowika huwa linamuasha mwenye nyumba kwamba
kumekucha…sasa wapinzani wametuamsha, na sasa hivi tumejipanga, hamtaamini
kitakachotokea kuanzia serikali za mitaa mpaka serikali kuu…”Alisema Wambura.
Aidha aliongeza kuwa katika ziara zake ambazo amekuwa akifanya katika
maeneo mbalimbali Mkoani Mwanza akiwa kama Mjumbe wa CCM Mkoa wa Mwanza,
amekumbana na vilio kutoka kwa wananchi wakiwa wanajutia kuwachagua wapinzani
wao katika maeneo yao hali ambayo inawapa imani Wafuasi wa CCM kuyarejesha
maeneo hayo mikononi mwao.
“Mfano nimezunguka katika Wilaya ya Ukerewe kama mjumbe wa kamati ya
utekeleza wazazi Mkoa, wale ambao walifanya makosa hayo ya kusema CCM tumechoka
ngoja tujaribu upande wa pili wanalia kilio ambacho huwezi kuamini mpaka
mwananchi mmoja akasema kwamba jamani CCM kama ni adhabu imetosha tunaomba basi
mtusikilize na sisi, tukawaambia kutenda kosa si kosa…” Alisema Wambura huku akibainisha kwamba wanainchi hao wanalia kutokana na kukosekana kwa huduma za msingi katika Wilaya hiyo baada ya Viongozi wa upinzani waliowachagua kushindwa kutekeleza wajibu wao ipasavyo.
Mjumbe huyo Alfred Wambura mbali ya kuwa Mjumbe wa Jumuia ya Wazazi wa
CCM Mkoa wa Mwanza pia ana nafasi nyingine nyingi ambazo anazisimamia ambazo ni
pamoja na mwenyekiti wa mtaa wa National Magharibi sanjari, mwenyekiti wa wenyeviti
wa Kata ya Nyakato wanaotokana na Chama cha Mapinduzi sanjari na kuwa Kamanda
wa UVCCM Kata ya Nyakato Wilayani Ilemela.
“Kazi yangu ya kwanza kabisa kwa vijana ni amani na utulivu kwa sababu
siku zote wavunja amani huwa ni vijana na hasa hawa wanaokariri wanaoambiwa tu maneno
ya kukariri wanaripuka bila kuyatathmini na kuyafanyia uchunguzi…” Alisema mzee
wa wambura baada ya kuchaguliwa kuwa kamanda wa UVCCM Kata ya Nyakato.
No comments: