LIVE STREAM ADS

Header Ads

MAKALA: UTEJA WA DAWA ZA KULEVYA UNACHANGIWA NA UNYANYAPAA TOKA KWA JAMII.

Tabia  ya  jamii  kuwanyanyapaa  watumiaji wa dawa za kulevya  imekuwa ikichangia  kwa kiasi  kikubwa  wateja   wa dawa   za kulevya  waliacha  kurejea  matumizi  ya  dawa  hizo na  matokeo   kuthidi  kuathirika  kimatendo  kiroho na kimwili.

Makala  hii  ilijikita  kutazama    mtazamo wa  jamii  juu  ya  
waliokuwa  wateja wa dawa za kulevya  baada  ya  kupata   program  maalumu  toka  kwenye  Nyumba  za utimamu   (Sober Houses)  na   wanaopata  tiba ya  methadone   toka kwenye kiliniki za Muhimbili, Mwanayamala  na  Temeke.

Ni  imani yangu  kuwa,  tiba  hizo  mbili  ni msaada  mkubwa kwa   wateja  wa  dawa  za kulevya,   endapo  mtu  atajitambua  na kujikubali  ni wazi  kuwa  ataachana  na  maisha  ya uteja  wa dawa za kulevya na kuishi  maisha  huru  bila kuwa  mtumwa  wa dawa za kulevya.

Jamii  ina wajibu mkubwa kwa waliokuwa wateja wa dawa za kulevya  katika  kuhakikisha kuwa hawanyanyapaliwi  ili  wasiweze kurudi tena  kwenye matumizi  ya dawa za kulevya  kwa kupata  upendo mkubwa  toka kwa  familia, ndugu na marafiki. Suala  hili  limekuwa  gumu  sana  kwa jamii, kwani watu wengi wamekuwa  hawana  imani  tena   kwa mtu  aliyekuwa akitumia dawa za kulevya  na  baadaye  kuamua  kuacha.

Bwana Novatus  William  mtumiaji wa dawa za kulevya  anayepata  tiba  ya utimamu wa mwili  ya  Pili  Missanah  Mwamza  alisema kuwa  mazingira  ya  awali  yana  nafasi kubwa  sana ya  kumrudisha  mtu aliyekuwa  mteja  wa dawa za kurejea  tena  kwenye  matumizi ya dawa za kulevya  kwa kuwa  jamii  inayomzunguka  ina  baki  na  picha  ile ile  ya  uhalifu kwa mtu  yule  yule. .

Naye  Bwana Nicholus  Manota toka  Nyumba  ya  utimamu  ya  pili Missah   alisema kuwa  familia  za  watu  waliokuwa  wakitumia  dawa za kulevya zinakosa    kurudisha imani  kwa   ndugu zao  wanapoacha   kutumia  dawa   za kulevya  baada  ya  kutoka  kwenye  nyumba  za utimamu  na  hali  hiyo  inapelekea  walioacha  dawa   kukosa   imani ya  kuheshimiwa  na jamii zao   na hali  hizo  zinapelekea   mtu  kurudi  katika  matumizi  ya  dawa  kwa lengo  la  kupata faraja.

Pia Manota aliongeza  kuwa,  hata  jamii  inayozunguka  nyumba  za utimamu (Sober  Houses) imekuwa  haina  imani  kabisa   kwa kudhani  wao ni wahalifu   wakati  ilibidi  watambue  kuwa  wao ni watu  wenye  matatizo ya  kiafya  kama  walivyo  wagonjwa wengine na  sio  wahalifu.

Naye  meneja wa  nyumba  ya  utimamu  ya   Pili Misanah  kata  ya  Ilongazala , wilaya ya  Ilemela   Jijini Mwanza   Bwana  Mohammed Mohammed  alibainisha  kuwa,  tatizo  kubwa  la wateja  wengi   walioacha  dawa  za kulevya  kurejea kwenye  matumizi  ya  dawa za kulevya  ni  kukosekana  kwa  ushirikiano  toka  kwa  jamii, kwani  jamii  imekuwa  haitaki  kuamini  kwamba  mtu  anayetumia  dawa za kulevya  anaweza kupona  na kurejea  katika  hali  yake  ya  kawaida. Kitendo  hicho  kimekuwa  kikiwabagua   wateja walioacha  dawa za kulevya  na  hatimaye  kujikuta wametengwa na jamii  nzima  na hapo  ndipo  urudi  kwenye   kwenye  matumizi  ya  dawa za kulevya  ili  kupata  faraja.

Naye   Daktari  wa Kiliniki  ya  methadone  ya  Muhimbili   Bwana  Kassian Nyandidi  alisema  kuwa,  mtumiaji wa dawa  za kulevya  ana  uwezo  wa kupona  kabisa  kutumia  dawa  za kulevya  kwa kutumia  njia  mbalimbali  kama  kunywa  methadone  au  kwenda  katika  nyumba  za utimamu  na  jamii  isiwatenge  watu  hao  walioonyesha    nia  ya  kuacha  kutumia  dawa za kulevya.

Nyandidi  aliongeza  kuwa   wateja  wa dawa za kulevya   upendo  wa  kijamii ili waweze kuimarika  kimwili  na  kiroho  na kujiona ni sehemu  ya  jamii  licha  ya maovu  waliyokuwa  wakiyafanya.

Naye  Bibi  Rehema  Abdallah  aliyeacha  dawa za kulevya kwa kuhudhuria Kiliniki  ya  Methadone  ya Muhimbili  alimwambia  mwandishi wa makala  hii kuwa,  dawa za kulevya zinauwezo wa  kuachwa  cha  msingi    ni  elimu  kwa  jamii  juu  ya  ukweli  huu, kwani  jamii bado  inamchukulia  mteja wa dawa za kulevya  sawa na  muhalifu.

Bwana  Leonard  Cyprian mkazi wa  Mabatini ,Wilaya ya Ilemela  Jijini Mwanza  alisema  kuwa  jamii    inaishi  na ndoto  za  vitendo  viovu  vilivyokuwa  vinafanywa  na  wateja  wa dawa za kulevya hasa  za  wizi  na  unyang’anyi  hivyo  inakuwa  vigumu  sana  kwa  mara  moja  kuamini  kuwa  mtu  aliyekuwa  mwizi  anaweza kuwa  mwema.

Ni wazi  kuwa  jamii  inabidi  ibadilike na kuamini kuwa  mtumiaji wa  dawa za kulevya  anaweza  kupona  na kurejea   katika maisha  yake  ya  kawaida, cha  msingi   jamii   iwe na  upendo  na  wale  wote  walioacha  kutumia dawa za kulevya, kwani  kuzidi  kuwanyanyapaa  ni kuzidi kukuza   tatizo   badala  ya  kupunguza  tatizo, iwachukulie  watu  hao  kama  wagonjwa  wengine  wa malaria  au  Virusi  vya Ukimwi/AIDS.

Kwa  ushauri wasiliana    na Mwandishi  wa makala  hii  kwa simu  0754551306
Makala  hii  imedhaminiwa  na   Mfuko  wa Kuvisaidia Vyombo  vya  Habari  Tanzania(TMF).

Na:  Edwin soko,

Mwanza.

No comments:

Powered by Blogger.