RATIBA YA KUUAGA MWILI WA ALIEKUWA KOCHA MSAIDIZI WA TIMU YA TAIFA SYLIVESTER MARSH YATOLEWA.
Na:George Binagi-GB Pazzo
Mwili
wa aliekuwa Kocha Msaidizi wa Timu ya Taifa ya Mpira wa miguu Sylivester Marsh
unatarajiwa kuagwa leo katika Uwanja wa Mirongo Jijini Mwanza, kabla ya
kwenda kuzikwa katika katika makaburi ya Igoma, baada ya kuwasili Jijini Mwanza jana jioni.
Akizungumza jana na Metro Fm & Binagi Media Group, Badrudin Nsubuga
ambae ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mazishi ya Marehemu Marsh, alisema kuwa shughuli
ya kuuaga mwili huo inatarajiwa kufanyika leo kuanzia majira ya saa 06:00
asubuhi hadi saa 12:00 mchana katika Uwanja wa Shule ya Msingi Mirongo, ambapo baadae
mwili wa marehemu Marsh utapelekwa nyumbani kwao Igoma kabla ya kwenda
kupumzishwa katika nyumba yake ya Milele katika Makaburi ya Igoma.
Mjane wa Marehemu Marsh Bi.Asha Sylivester Marsh alielezea kupokea
kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa Marehemu Mars ambapo amebainisha
kuwa bado alikuwa akimhitaji zaidi Marsh kwa ajili ya malezi ya watoto ambao
bado ni wadogo na wanasoma.
Zaidi aliwahusia wanamichezo nchini kufuata nyayo za Marehemu
Marsh katika utendaji wake wa kazi sanjari na kuwapenda na kuwashauri vyema
watu wote kubwa zaidi kupenda kuibua na kuendeleza vipaji kwa wanamichezo kama
Marehemu Marsh alivyokuwa akifanya.
Nae Jumaine Shengelo ambae ni Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Soka
Mkoa wa Mwanza MZFA alimuelezea Marehemu Mwalimu Marsh kuwa katika enzi za uhai
wake wakati akicheza mpira, alikuwa ni kijana mtulivu na mwenye nidhamu
uwanjani ambae alikuwa na mwamko wa kimichezo hali iliyomsukuma pia kuanzisha
kituo cha michezo pamoja na Timu ya Soka ya Marsh Athletic Academy.
Aidha aliongeza kuwa jambo ambalo angependa kuliweka wazi ni
kwamba Timu ya Marsh Athletic Academy haitakufa, kwa sababu ameacha watu ambao
wataweza kuiendeleza kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
Nae Samiry Omary ambae ni Mchezaji wa timu ya Soka ya Marsh
Athletic Academy alisema kuwa wachezaji wa timu hiyo wameupokea kwa masikitiko
makubwa msiba wa Marehemu Mwalimu Marsh kwa kuwa bado walikuwa wakimhitaji na
walikuwa wameahidiana mambo mengi ya kimichezo ambapo wamewaomba wadau michezo
wajitokeze katika kuiendeleza aliyoiacha ya Marsh Athletic Academy.
Akizungumza kwa masikitiko Makubwa Hamza Yusuph Shido ambae ni
Mdau wa Michezo na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Utemini Kata ya Mirongo
ulipo Msiba wa Marehemu Mwalimu Marsh, alisema kuwa wanamichezo wamesikitishwa
kwa kitendo cha mwili wa Marehemu Mwalimu Marsh kusafirishwa kwa njia ya
barabara (Kwa gari/ Coaster) kutoka Jijini Dar es salaam ukilinganisha nafasi
aliyokuwa nayo katika Soka la Tanzania.
Alisema amesikitishwa namna Chama cha Soka Mkoani Mwanza MZFA
pamoja na Shirikisho la Soka nchini TFF walivyoshindwa kumuenzi Marehemu
Mwalimu Marsh hususani kwa namna mwili wake ulivyosafirishwa sanjari na katika
michezo ya ligi kuu ya Tanzania bara iliyochezwa jana kushindwa kuonyesha
ishara ya aina yoyote ya kumuenzi marehemu Marsh.
BINAGI MEDIA GROUP: PUMZIKA KWA AMANI KOCHA MZALENDO MARSH.
No comments: