LIVE STREAM ADS

Header Ads

MANSOOR AWAHIMIZA WANANCHI WA HUNGUMALWA KUJIANDIKISHA ILI KUUNGANISHIWA NISHATI YA UMEME.

Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (Kushoto) akiwakabidhi walengwa mifuko ya Simenti iliyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Kwimba Sharif Hiran Mansoor (mwenye Kinasa sauti).
Na:George GB Pazzo
Mbunge wa Jimbo la Kwimba Mkoani Mwanza Sharif Hiran Mansoor (CCM) amewahimiza Wananchi wa Kata ya Hungumalwa Jimboni humo, kujiandikisha kwa wingi ili kuunganishiwa nishati ya Umeme baada ya nishati hiyo kufikishwa katika Vijiji vya Kata hiyo.

Mansoor alitoa kauli hiyo ijumaa iliyopita wakati wa Uzinduzi wa Umeme katika Vijiji vya Kata ya Hungumalwa, ambapo alibainisha kwamba kwa juhudi zake nishati hiyo ya Umeme imefikishwa katika Kata ya Hungumalwa kupitia Mpango wa Umeme Vijijini.

Alisema kuwa kasi ya wananchi kujiandikisha kwa ajili ya kufikishiwa huduma ya Umeme katika Kata hiyo ni ndogo ambapo alibainisha kuwa Kaya 65 pekee ndizo zimeweza kujiandikisha na kulipia gharama za kuunganishiwa Umeme, ambapo kwa kila kaya gharama ya kuunganishiwa Umeme ni shilingi 27,000 pekee.

Kuhusu kero ya Maji katika Jimbo la Kwimba, Mansoor alieleza kuwa kero hiyo imekwisha tafutiwa Ufumbuzi ambapo tayari Mradi wa Maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka Maji Jimboni humo umekwisha kamilika hivyo kilichosalia ni Maji hayo kuanza kusambazwa kutoka katika tenki la Maji lililopo Muhalo ili kuwafikia wananchi.

Mbali na hayo, pia Mansoor alikabidhi Mifuko Mia Sita ya Simenti kwa ajili ya shughuli mbalimbali za Maendeleo katika Kata ya Hungumalwa, Shilingi Milioni Tano kwa ajili ya Kusaidia kukamilisha Ujenzi wa Zahanati ya Kata hiyo, Shilingi laki tano kwa ajili ya Matibabu ya Mtoto mmoja alifikishwa na mzazi wake katika kikao cha halmashauru kuu ya CCM Wilayani humo pamoja na kuvisaidia vukundi vya ujasiriamali vya Mlimani, Ilungu, Buyogo na Tusaidiane Hungumalwa Vyelehani viwili kwa kila kikundi kwa ajili ya Shughuli zao za Ushonaji.

Akizungumza katika Uzinduzi huo wa Umeme katika Kata hiyo ya Hungumalwa, Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu alibainisha kuwa Chama hicho kimedhamiria kufikisha maendeleo kwa wananchi huku akiongeza kuwa chama hicho kimejengeka katika misingi ya watu tofauti na vyama vingine ambavyo amesema vimejengeka katika misingi ya Saccos na havina dhamira ya kuwatumikia wananchi.

Nao wananchi wa Kata ya Hungumalwa wamemshukuru Mbunge wao Mansoor kwa kutimiza ahadi yake ya kuwafikishia nishati ya Umeme ambapo wamebainisha kuwa mbali na matumizi ya nyumbani pia nishati hiyo itawanufaisha katika shughuli mbalimbali za uzalishaji pamoja na kuwasaidia wanafunzi kupata mwanga bora kwa ajili ya kujisomea na hivyo kuondokana na kero ya mwanga wa vibatari ambao ulikuwa ukiwaathiri hapo awali.
Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (mwenye miwani) akiwakabidhi walengwa mifuko ya Simenti iliyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Kwimba Sharif Hiran Mansoor (mwenye Kinasa sauti mkononi).
Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (Kushoto) akiwakabidhi walengwa vyelehani vilivyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Kwimba Sharif Hiran Mansoor.
Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (Katikati) akiwakabidhi walengwa vyelehani vilivyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Kwimba Sharif Hiran Mansoor.
Wananchi wa Hungumalwa wakiwa katika Mkutano wa hadhara uliofanyika ijumaa wiki iliyopita kabla ya uzinduzi wa Umeme katika Kata hiyo.
Msafara wa Mbunge wa Jimbo la Kwimba Sharifu Hirani Mansoor pamoja na Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu ukielea katika zoezi la Kuwasha Umeme kama ishara ya Uzinduzi wa Umeme katika Vijiji vya Kata ya Hungumalwa Wilayani Kwimba.
CREDIT: RADIO METRO MWANZA

No comments:

Powered by Blogger.