HOSPITALI YA RUFAA BUGANDO KUENDESHA ZOEZI LA UPASUAJI KWA WATOTO WENYE TATIZO LA VICHWA KUJAA MAJI.
Hospitali ya Rufaa Bugando ikishirikiana na Asasi isiyo ya kiserikali ya Marafiki wa Watoto wenye Saratani Tanzania na wafadhili mbalimbali, kesho inatarajia kuanza zoezi la upasuaji kwa Watoto wapatao 30, wanaosumbuliwa na ugonjwa wa Vichwa kujaa maji na mgongo wazi.
Hayo yalibinishwa na Mkurugenzi wa huduma za hospitali hiyo Prof.Japhet Gilyoma katika mkutano na waandishi wa habari jana uliofanyika katika ukumbi wa hospitli hiyo na kuongeza kuwa tatizo hilo limekuwa likiongezeka kila mwaka kutokana na jamii kutokuwa na uelewa kuhusu ugonjwa huo ambapo kwa takribani miaka minne iliyopita watoto 1081 wenye tatizo hilo wamefanyiwa upasuaji hospitalini hapo.
Pia alisema malengo ya hospitali hiyo ni kuhakikisha inakabiliana na tatizo hilo ,kwani tayari imeanzisha kambi maalum itakayokuwa inawafanyia upasuaji watoto wapatao 50 kila baada mwezi mmoja.
"Kadri mtoto anavyochelewa kutibiwa, ubongo nao unazidi kupungua, hivyo lengo letu ni kuhakikisha kuwa hadi kufikia desemba 2017 mtoto akifika leo hospitali kesho anafanyiwa upasuaji, hivyo tutaokoa maisha ya watoto wengi na kuondoa vilema vya kudumu. Alisema Prof.Gilyoma.
Aliongeza kuwa ili kukabiliana na tatizo hilo, Hospitali ya Bugando itaziwezesha hospitali zingine ili ziwe na uwezo wa kutibu ugonjwa huo na hivyo kupunguza ukubwa wa tatizo hilo katika utoaji wa huduma zake.
Naye Daktari wa Idara ya Upasuaji Bugando Dr. Gerald Mayaya alisema zaidi ya watoto 40,000 nchini huzaliwa wakiwa na tatizo la kichwa kujaa maji na mgongo wazi lakini kati yao 10,000 ndiyo wanaoenda hospitalini kupatiwa matibabu huku 3,000 wakiwa hawajulikani walipo.
Mariana Wiza ambae ni mmoja wa wazazi wenye watoto wanaosumbuliwa na tatizo la kichwa kujaa maji, aliwaomba wazazi na jamiii yenye watoto ambao wanasumbuliwa na tatizo kama la mtoto wake waache kuwaficha na badala yake wajitokeze na kuwapeleka hospitalini kwani kwani matibabu yake yanapatikana.
No comments: