LIVE STREAM ADS

Header Ads

Ukosefu wa zahanati unavyo watesa wajawazito wilayani Magu

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Na Blandina Aristides, Mwanza
Mipango mikakati na matamko mbalimbali ya viongozi wa serikali ni miongoni mwa mambo makuu ambayo huaminiwa  na wananchi kwa kiasi kikubwa katika nchi nyingi za Afrika.

Matamko hayo ambayo hutolewa kupitia nyaraka za serikali na za kuaminika, yanawapa matumaini wananchi na kuamini kuwa, kupitia hayo, changamoto zilizopo katika jamii zitapungua ama kuondolewa kabisa.

Tunaposema Matamko, ni azma ya serikali inayoelekeza kufikisha malengo iliyojiwekea kwa wananchi, kupitia nyaraka mbalimbali  kama vile sera, katiba, malengo endelevu ya kidunia na sheria.

Kutotekelezeka kwa baadhi ya ahadi ama maazimio yanayotolewa na viongozi wa serikali  kunawafanya watanzania  walio wengi kutoiamini serikali yao huku wakijiaminisha kuwa, imeshindwa kutekleza sera ambayo ndio matamko yenye kusudi la kufikia lengo na madhumuni maalum yaliyo kusudiwa.

Sera ya afya ya mwaka 1990 na kufanyiwa marekebisho mwaka  2007 kipengere cha 5.4.1 (b) kinaeleza kuwa serikali itaendelea kusogeza huduma za afya karibu na wananchi kwa kujenga zahanati katika kila kijiji na kituo cha afya katika kila kata lakini hali ilivyo sivyo inavyoelekeza.

Tangu kutungwa kwa Sera hiyo, mpaka sasa Vijiji vya Jinjimili na Kabale wilayani Magu havina zahanati hivyo kuwalazimu wananchi kutembea umbali wa zaidi ya kilometa 10 kufuata huduma za afya  katika kijiji cha Kabila.

Takwimu toka Hospitali ya wilaya ya Magu zinaonesha kuwa  taklibani  wakinamama 302 kwa mwaka 2015/2016 walijifungulia nyumbani  na wengine njiani jambo ambalo ni hatari kwa afya.

Takwimu hizo pia zionaonesha kuwa kati ya wanawake 1607 walioanza kliniki kwa kipindi cha Julai 2015-Septemba 2016, wanawake 302 walijifungulia nyumbani na baadhi yao njiani bila kuwa na msaada wowote kutoka kwa wauguzi ama wahudumu wa afya.

Hali hiyo imepelekea baadhi ya akinamama kukumbwa na magonjwa mbalimbali kamavile Kifafa cha mimba, Fistula na homa kali pale wanapofika kituoni baada ya kukaa muda mrefu nyumbani wakiwa wamejifungua.

Pamoja na Sera ya Afya ya Mwaka 2007, kueleza kuwepo na zahanati katika kila kijiji,  lakini mpaka sasa vijiji zaidi ya 40 katika Wilaya ya Magu, havina zahanati, hivyo kulazimika kutembea umbali wa taklibani kilometa 8-12 kwa ajili ya kupata huduma za afya iwe wakati wa jua ama mvua.

Bahati Katoro ni Kaimu Mtendaji wa kijiji cha Jinjimili ambaye anaeleza kuwa asilimia 65 ya wananchi , hupata huduma katika kata jilani ya Kabila kutokana na kutokuwepo huduma za afya maeneo ya karibu tangu kuanzishwa kwa vijiji hivyo huku asilimia 35 wakipata huduma katika kata ya Nyasato.

Takwimu kutoka katika ofisi ya  kijiji cha Jinjimili zinaeleza kuwa kata ya Jinjimili inawakazi 13,690 na kaya 1672 ambazo hulazimika kufuata huduma katika kituo cha afya cha Kabila kilichopo kwenye kata ya Kabila yenye wakazi 15,416 na kaya zaidi ya  1000.

Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka vigezo na taratibu za kuanzishwa na  kupandisha hadhi mamlaka za serikali za mitaa ambazo huanzishwa kwa kuzingatia Ibara ya 145 na 146  zinaelekeza kuanzishwashwa kwa vyombo vya Serikali za Mitaa katika eneo la Mikoa, Wilaya, Mji na Kijiji.

Katiba hiyo, imeweka pia  vigezo vya kuzingatia katika kuanzisha maeneo mapya ya utawala ngazi za chini za serikali za mitaa ambapo inaeleza kuwa Kitongoji kinatakiwa kuwa na Kaya zisizopungua 50 huku Kifungu cha 30 cha Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) kikielekeza kwamba eneo la Kijiji litagawanywa katika Vitongoji visivyozidi vitano.

Lakini pia imeweka vigezo vya kuanzisha kijiji ambapo inaeleza kuwa kila kijiji kinatakiwa kuwepo kwa eneo la kutosha kwa ajili ya matumizi ya wananchi kwa sasa na baadaye, vitongoji visivyopungua vitano, Idadi ya kaya zisizopungua 250, Idadi ya watu wasiozidi 10,000 na upatikanaji wa huduma za jamii kama vile maduka ya rejareja yasiyopungua matano (5), soko, shule ya msingi, zahanati na kituo kidogo cha polisi.

Mpaka sasa idadi ya watu waliopo katika vijiji vya Jinjimili na Kabale, ni kubwa ikilinganishwa na katiba inavyoelekeza lakini pia hata idadi ya kaya zilizowekwa kwenye katiba, ni tofauti na hali ilivyo katika vijiji hivyo.

Kaimu Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Jinjimili, Bahati Balisondole anaelezea kuwa wanawake katika kijiji hicho wanapo tembea umbali huo hutumia muda mrefu, wakati huo hata eneo wanakokwenda kupata huduma huzipata wakiwa wamechelewa kutokana na wingi wa watu waliopo.

Aidha wanatumia taklibani zaidi ya saa mbili mpaka kufika kituoni na wakati mwingine hupoteza kuda huo kwenda kituoni na wasipate huduma walizotakiwa kupata.

Uchunguzi umebaini, muda wanaoutumia kufuata huduma za afya, hata nguvu kazi ya uzalishaji mali inakua ndogo, kwani muda mwingi wanautumia kutembea huku shughuli nyingine zikiwa zimesimama.

Sesilia Peter, ni mmoja wa akina mama ambaye alieleza kuwa, wakati mwingine hutumia wakunga wa jadi pale hali inapoonekana kuwa mbaya, lakini pia haisaidii kwani wakati mwingine hata mkunga, anashindwa kuwasaidia pale tatizo linapoonekana kuwa kubwa zaidi.

Sesilia ambaye alikutana na mwadishi wa makala hii, wiki mbili baada ya kujifungua akiwa njiani kuelekea hospitali, alieleza kuwa baada ya kupata uchungu, alitafuta usafiri wa baiskeli ili iweze kumfika kituoni, lakini hali ilibadilika akiwa njiani na hatimaye akajifungua bila kufika eneo husika.

Stela Samweli ni mama wa familia yenye watoto watatu nanimiongoni mwa  mama wajawazito ambao, hajawahi kujifungua katika kituo chochote cha afya, badala yake amekua na mazoea ya kujifungulia nyumbani siku zote kutokana na kutokuwa na uwezo wa kulipia usafiri wa kumfikisha kilipo kituo cha afya cha kutolea huduma.

 “Tangu niolewe nikaanza kupata watoto, kujifungulia hospitalini  kwangu ni kama ndoto, na nina watoto watatu mpaka sasa, lakini pia sijapatwa na tatizo lolote,” anasema Stela.

Marco Samweli, ni Muuguzi katika kituo cha afya cha Kabila ambaye ameeleza kuwa, kutokuwepo kwa zahanati katika baadhi ya vijiji wilayani Magu, kumesababisha ongezeko la watu katika kituo hicho wanaokuja kupata huduma.

Kituo hicho  kimekua kikipokea wagonjwa kutoka vijiji vya Jijnjimili, Kabale, Kabila, Shishani, Nkungulu na Ng’haya, huku baadhi ya wananchi wengine wakitoka wilaya jirani za Kwimba na Bariadi mkoani Simiyu.

Taarifa za kituo cha afya cha Kabila zinaonyesha kuwa, kwa siku kina uwezo wa kupokea wajawazito zaidi ya 10, watoto wanaoletwa kliniki zaidi ya 25, wanaotibiwa na kurudi nyumbani zaidi ya 15 na pia wana uwezo wa kupokea takribani wanawake sita walioko katika hatua ya kujifungua.

Hali hiyo inawapa wakati mgumu kwani hata wahudumu wanaokuwa zamu, ni wawili tu jambo ambalo huwafanya kuwa na kazi nyingi kwa wakati mmoja.

Baadhi ya wanawake hukabiliwa na magonjwa mbalimbali ikiwa ni pamoja na fistula, malelia kali, magonjwa ya moyo, mimba kuharibika na kwamba wengine hukutwa magonjwa hayo yamewaathili kwa kiasi kikubwa.

Idadi hiyo ya watu wanaopata huduma kituoni hapo, ni kubwa ikilinganishwa na watumishi waliopo, kwani wakati mwingine huwalazimu kutumia muda wa ziada ili kuhakikisha wananchi wanapatiwa huduma stahiki na kurudi majumbani mwao.

Kwa mujibu wa Marcko ambaye ni muuguzi kituoni hapo, kituo kina Daktari mmoja, matabibu wawili, wauguzi wa nne na mabwana afya wawili huku akieleza kuwa hata uwezo wa wodi ya akinamama ni mdogo kwani inavitanda saba yu vya kujifungulia.

Anafafanua kuwa, hata vitanda hivyo vimebanana na wakati mwingine inawabidi kuchukua magodoro kutoka wodi nyingine ya wagonjwa  wa kawaida na kuyaweka chini ili kuhakikisha wamama hao wanapata nafasi ya kupumzika  na watoto wao baada ya kujifungua.

Pamoja na suala la kutokuwepo kwa zahanati katika vijiji hivyo, vilevile kuna idadi kubwa ya akina mama ambao hawana upeo mkubwa wa elimu ya kutosha juu ya upatikanaji wa huduma bora ya uzazi kwa mama mjamzito na hivyo, kujikuta wakiendeleza desturi, mila na mazoea ya kujifungulia nyumbani badala ya kufika katika vituo vya afya ama zahanati.

Hali hiyo ni kawaida katika vijiji hivyo, wakisahau kuwa kufanya hivyo, ni kuhatarisha afya zao kwa sababu huduma anayotakiwa kupatiwa mama baada ya kujifungua, hawazipati kutokana na mazingira aliyojifungulia.

Charless Lutonja ambaye naye ni mkazi wa kijiji hicho anaeleza kuwa hali ya wananchi wa kijijini sio nzuri kwani hata usafiri wa kuweza kuwasaidia ili kupata huduma haraka ni shida.

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Magu, Maduhu Nindwa alieleza kuwa chanzo kikuu ni uelewa mdogo kwa baadhi ya akina mama juu ya nini afanye mara tu anapogundua kuwa na ujauzito.


 “Jamii bado ina uelewa mdogo kwenye umuhimu wa maandalizi ya kuzuia matatizo kama hayo ya kujifungulia njiani ama nyumbani, kwani  maandalizi yanatakiwa yaanze mwanzo angalau miezi sita kabla ya muda wa kujifungua kufika na ikiwezekana toka siku anayojua amepata mimba,” alibainisha Dr. Nindwa.
Baadhi ya wakinamam wa kijiji cha Jinjimili  wilayani Magu, wakieleza adha wanayokumbana nayo kutokana na umbali mrefu  uliopo kutoka nyumbani hadi kilipo kituo cha afya.

No comments:

Powered by Blogger.