LIVE STREAM ADS

Header Ads

Hospitali ya Mkoa Mbeya yakabiliwa na changamoto ya mtambo wa kuteketeza taka

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com

Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mussa Sima (wa pili kutoka kushoto) akitoa maelekezo kwa Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya , Dkt. Paul Lawala baada ya kutembelea Hospitali hiyo kukagua namna taka ngumu na hatarishi zinavyoteketezwa. 
Shimo ambalo linatumika kwa sasa kuteketeza taka za Hospitali ya Rufaa ya Mbeya baada ya mtambo maalum wa kutetekeza taka hizo kuwa katika hatua za ukarabati. Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mussa Sima amemuagiza Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, Dkt. Paul Lawala kuandaa mkakati wa haraka wa kupata mtambo mpya (Incinerator) wa kuteketeza taka hatarishi.
Mtambo wa kuteketeza taka wa Hospitali ya Rufaa ya Mbeya kama unavyoonekana ukiwa katika hali chakavu na ukifanyiwa ukarabati. Katika ziara ya kikazi, Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mussa Sima ameagiza kukarabatiwa kwa mtambo huo mapema iwezekanavyo kama hatua za haraka na kutafuta kiteketezi taka ambacho kitakidhi mahitaji ya Hospitali ya Rufaa.

Na Lulu Mussa, Mbeya 
Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya imeagizwa kuja na mpango mkakati wa haraka wa kukarabati mtambo maalum wa kuteketeza taka hospitalini hapo badala ya kutumia mfumo wa sasa wa kuchoma taka hizo katika shimo kitendo ambacho ni uchafuzi wa mazingira na kinahatarisha afya za wagonjwa na wakazi wa maeneo jirani kutoka na kukithiri kwa moshi. 

Katika ziara yake mkoani Mbeya yenye lengo la kukagua maeneo yenye changamoto za kimazingira katika sekta ya afya na namna ya uteketezaji wa taka pamoja na kuzitafutia ufumbuzi, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mussa Sima ameshuhudia kukosekana kwa mtambo maalumu wa kuteketeza taka Hospitalini hapo na uteketezaji wa taka kufanyika katika shimo ambalo si salama kiafya na kimazingira. 

"Nimeshuhudia Hospitali ya Rufaa ya Mbeya haina Incinerator, taka hatarishi zinachomwa kwenye shimo bila tahadhari yoyoye, kuna madhara makubwa zaidi ya uchomaji wa taka katika eneo hilo. Kama hatua za haraka nimeagiza taka hizo ziteketezwe katika burning chambers na waanze kuweka mkakati wa kupata incinerator itakayokidhi mahitaji". Sima alisisitiza. 

Waziri Sima amesema uchomaji wa taka hususan taka hatarishi bila kuzingatia taratibu madhara yake ni makubwa hasa kwa jamii inayozunguka, ukizingatia hospitali hiyo inapakana na Shule ya Sekondari ya Loleza. Ameelekeza kusitishwa kwa uchomaji taka wa aina hiyo na badala yake uongozi wa Hospitali hiyo utumie kiteketezi taka maalumu "burning chambers" kama mkakati wa haraka ili kunusuru afya za watu na mazingira. 

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Mussa Sima ameshuhudia kiasi kikubwa cha taka ngumu ambazo hazijazolewa hospitalini hapo kwa kipindi kirefu na kusababisha hofu ya mlipuko wa magonjwa. Katika kutatua changamoto hii Naibu Waziri Sima ameagiza Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya na Uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mbeya kukaa pamoja na kuweka mkakati endelevu wa kuhakikisha taka zinaondolewa kwa wakati Hospitalini hapo. 

Alipoulizwa juu ya hali hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya, Dkt. Paul Lawala amekiri kuwa Hospitali hiyo inakabiliwa na changamoto ya uzoaji taka kwa wakati na kuainisha kuwa changamoto hizo zinafanyiwa kazi ikiwa ni pamoja kuanza kwa ukarabati wa ‘burning chamber’ na mkakati wa kupata mtambo maalumu wa kuteketeza taka utakaokidhi mahitaji halisi.

No comments:

Powered by Blogger.