LIVE STREAM ADS

Header Ads

RC Singida: Ukamilishaji wa miradi ya maendeleo ni jambo la kufa na kupona

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba akizungumza na viongozi mbalimbali wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida wakati alipokuwa akikagua mradi wa ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Mkhandi kilichopo wilayani humo leo May 30, 2023. Kulia ni Mkuu wa wilaya hiyo, Mhandisi Paskas Muragili na kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Omari Mande.

Na Dotto Mwaibale, Singida
Mkuu wa Mkoa wa Singida,Peter Serukamba amesema kazi ya kumalizia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika wilaya zote mkoani hapa ni la kufa na kupona na kuwa kazi hiyo ifanyike usiku na mchana kutokana na umuhimu wake.

Serukamba ameyasema hayo leo May 30, 2023 wakati alipokuwa katika mwendelezo wa ziara yake ya kutembelea na kukagua ukamilishaji wa miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida na kuhimiza miradi yote iwe imekamilika kabla ya Julai 1, 2023 kwa viwango vinavyotakiwa na kulingana na thamani halisi ya fedha zilizotolewa.

" Mkurugenzi, Mkuu wa wilaya, Madiwani, Mhandisi na timu yenu nzima msikae ofisini nendeni ilipo miradi na hakikisheni ukamilishaji wake unakuwa ndani ya siku 20 kuanzia leo na si vinginevyo kwani fedha zote zitakazo salia kabla ya kuikamilisha zitarudishwa serikalini mwisho wa mwaka wa fedha wa 2022/ 2023 ambapo zimebaki siku 20 tu kuanzia leo,” alisema Serukamba.

Serukamba alisema hatapenda kuona fedha hizo zikirudi bila ya kumaliza kazi iliyokusudiwa ya kumaliza ujenzi wa miradi hiyo yakiwemo madarasa, zahanati na mabweni kwani kurudi kwa fedha hizo Rais Dk. Samia Suluhu Hassan aliyezitoa hatakuwa ajatendewa haki pamoja na wananchi ambao ndio walengwa wa miradi hiyo.

Aidha, Serukamba alisisitiza vituo vya afya na zahanati zinazoendelea kujengwa ujezi wake uwe umekamilika kabla ya Julai na Julai Mosi, 2023 zizinduliwe rasmi na kuanza kutoa huduma za afya kwa wananchi.

Alisema agizo la kukamilisha miradi hiyo kabla ya Julai, 1, 2023 kwa halmashauri zote nchini zimetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Angellah Kairuki na ndio maana wapo katika ziara ya kuhimiza kukamilika kwa miradi hiyo.

Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Omari Mande akizungumza kuhusu utekelezaji wa miradi hiyo alisema maagizo yote aliyoyatoa Mkuu wa Mkoa watayatekeleza kama walivyoagizwa na kuwa hakuna mradi hata mmoja ambao hautakamilika ndani ya muda huo.

Miradi aliyoitembelea leo ni ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Makhandi ambayo ujenzi wake ulianza mwaka 2019 kwa nguvu za wananchi kwa ushirikiano wa vijiji viwili vya Makhandi na Idd Simba, ujenzi wa bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari ya Maghojoa ambapo Mkuu wa Mkoa Serukamba aliomba halmashauri hiyo itumie fedha zake za ndani kwa ajili ya kuingiza umeme na maji.

Mradi mwingine uliokaguliwa ni ujenzi wa Zahanati ya Kijijicha Sagara, ujenzi wa bwalo la chakula katika Shule ya Sekondari ya Itaja, Ujenzi wa vyoo katika Shule ya Msingi ya Mwighanji, ujenzi wa bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari ya Mughanga, ujenzi wa bweni kupitia mradi wa elimu maalum.

katika Kijiji cha Mgori, ujenzi wa darasa katika Shule ya Msingi Mughamo na ujenzi wa nyumba ya walimu katika Shule ya Msingi Ngaramtoni.

Katika ziara hiyo Serukamba aliongoza na wakuu wa idara, maafisa watendaji wa kata na Tarafa, wataalam na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya hiyo.

Kesho Mkuu wa Mkoa Peter Serukamba anatarajia kuendelea na ziara yake hiyo katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo na kuhimiza ukamilishwaji wake kwa wakati.
Mkuu wa wilaya hiyo, Mhandisi Paskas Muragili, akisisitiza jambo wakati wa ukaguzi wa Zahanati ya kijijihicho.
Muonekano wa zahanati ya kijiji hicho.
RC Serukamba akisisitiza jambo kwenye ziara hiyo.
Muonekano wa zahanati ya Kijiji cha Sagara wakati wa ziara hiyo.
Ukaguzi wa Zahanati ya Kijiji cha Sagara ukifanyika.
RC Serukamba akielekeza jambo baada ya ukaguzi wa zahanati ya Kijiji cha Sagara.
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, akizungumza wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa Bwalo la Shule ya Sekondari ya Itaja.
Muonekano wa ujenzi wa Bwalo hilo.
RC Serukamba akiwa ameongoza na Diwani wa Kata ya Itaja, Paul Himida wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa Bwalo hilo
Ukaguzi wa ujenziwa vyoo vya Shule ya Msingi,Mwighanji ukifanyika.
Muonekano wa vyoo vya Shule ya Msingi, Mwighanji ambavyo vilikuwa vikitumika.
Ukaguzi wa ujenzi wa nyumba ya walimu katika Shule ya Msingi Ngaramtoni ukifanyika.
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Omari Mande akielekeja jambo wakati wa ukaguzi wa ujenzi nyumba hiyo ya walimu.
Muonekano wa bweni la wanafunzi wasichana wa Shule ya Sekondari ya Mughanga ambao ujenzi wake umekamilika. RC Serukamba ameomba washirikishwe wazazi ili waweze kununua vitanda na vifaa vingine ikiwa ni pamoja na kuingiza maji ili wanafunzi hao waanze kulitumia bweni hilo.
Ukaguzi wa bweni kwa ajili ya watoto maalum linalojengwa Kijiji cha Mgori ukiendelea.
Muonekano wa bweni hilo ambalo ujenzi wake upo mwishoni kukamilika.
Ukaguzi wa ujenzi wa darasa katika Shule ya Msingi Mughamo ukifanyika.

No comments:

Powered by Blogger.