LIVE STREAM ADS

Header Ads

Waumini wa kiislamu wafurahia sadaka ya nyama wakiadhimisha Eid Al- Adha

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Uchinjaji wa Ng'ombe kwa ajili ya sadaka ya Eid Ul Adha ukifanyika katika kituo cha Nuru Islamic Foundation Manispaa ya Singida Juni 28, 2023

Na Dotto Mwaibale, Singida
Waislamu Singida wamepongeza utaratibu uliotumika kugawa wanyama waliochinjwa kwa ajili ya kusherehekea Sikukuu ya Eid Ul Adha ambayo inafanyika leo duniani kote.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa ugawaji wa wayama hao mjini hapa walisema zoezi hilo kwa mwaka huu limeratibiwa vizuri kwani waislam na wananchi wengi wamepata sadaka hiyo tofauti na mwaja ambapo licha ya wanyama hao kuwa wengi kulikuwa na ujanja ujanja uliosababisha wengi wao kukosa.

Mkazi Mungumaji katika Manispaa ya Singida, Amina Hamadi alipongeza utaratibu uliofanyika wa ugawaji wa sadaka hiyo kwa kusema mwaka jana hakupata kabisa licha ya kuwepo jirani na kambi ya uchinjaji maeneo ya Karakana.

“Mwaka jana nilishinda kutwa nzima nikiwa na wenzangu lakini hatukupata sadaka hii lakini leo tumepata mbuzi mmoja tugawane watu wawili jambo ambalo sikulitegemea kabisa,” alisema Amina.

Abubakar Ntandu aliyekuwepo kwenye zoezi hilo alisema utaratibu uliofanywa na Taasisi ya uchinjaji wa wafanyama hao ya Arrayan ya kuchinja na kupeleka vijijini kwa kutumia magari imesaidia waislam wengi waishio pembezoni mwa mji wa Singida na vijiji jirani kupata sadaka hiyo.

“Safari hii nafikiri taasisi hizi zinazochinja kwa kushirikiana na Ofisi ya Baraza Kuu la Waislam Tanzania (BAKWATA) Mkoa wa Singida zilijifunza kitu baada ya kuwepo malalamiko ya baadhi ya watu na viongozi wa dini hiyo ambao walikuwa wakichukua wanyama wengi lakini walikosa uaminifu na kujinufaisha wao kwa kuiuza badala ya kuwafikishia walengwa,” alisema Ntandu.

Msimamizi wa Taasisi ya Arrayan inayojishughulisha na uchinjaji wa wanyama kwa ajili ya sadaka, Ally Shabani alisema utaratibu wa mwaka huu wa kuchinja wanyama hao na kuwapekeka nje ya mji umeleta mafanikio makubwa kwani umepunguza malalamiko ya watu kukosa sadaka hiyo.

“Mwaka huu kila mtu aliyefika eneo la uchinjaji amepata sadaka tunamshukuru Allah katika jambo hili,” alisema Shabani.

Shabani alitoa wito kwa waislam watakaopata sadaka hiyo wakati wa zoezi hilo ambalo litaendelea leo kuwa na moyo wa upendo wa kuwapatia na wenzao hata kilo moja au mbili badala ya mtu mmoja kung’ang’ania apate nyama nyingi peke yake.

Mapema juzi Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro alitoa onyo kwa mtu au kiongozi yeyote wa kiislam ambaye angebainika kuiba wanyama hao kuwa angekamatwa kwani angekuwa sawa na wezi wengine hivyo angepelekwa polisi.

Hata hivyo baadhi ya wafanyabiashara wa bucha walitoa tahadhari na kulalamikia uchinjaji holela kila sehemu kuwa umekuwa ukileta changamoto katika biashara yao kutokana na mauzo kuwa chini na kujikuta wakiingia hasara.

Kwa upandewake Twalib Omari Masika ambaye ni msimamizi wa uchinjaji katikakambi ya Karakana alisema shughuli hiyo ya kuchinja wanyama hao ni sadaka inayotolewa baada ya Hija kama suna kwa waislam na wasio wa waislam kwa ajili ya kusherehekea Sikukuu hiyo ya Eid Ul Adha.

“Tuna wachinja wanyama hawa na kuwapakia kwenye magari ambayo tumeyakodi na kuwapeleka vijijini ambako kuna watu wengi wenye uhitaji tofauti na hapa mjini,” alisema Masika.

\ alisema katika ugawaji wa wanyama hao taasisi hiyo imeweka utaratibu wa wahitaji wote kuandikwa majina na jeshi la polisi na askari binafsi ndio waliosimamia usalama.

Baadhi ya Taasisi zilizopongezwa kwa kuratibu zoezi hilo vizuri ni ya Arrayan, Nuru Islamic Foundation zikiwemo na nyingine mbalimbali.
Uchinjaji ukiendelea katika kituo hicho.
Msimamizi wa Taasisi ya Arrayan inayojishughulisha na uchinjaji wa wanyama kwa ajili ya sadaka, Ally Shabani, akizungumza na wanawake wa Kiislam waliofika kupata sadaka hiyo katika kituo cha uchinjaji cha Karakana kilichopo nje kidogo ya Manispaa ya Singida.
Msimamizi wa uchinjaji wa Taasisi ya Nuru Islamic Foundation, Ramadhan Juma, akielezea zoezi zima la uchinjaji katika kituo hicho.
Mkuu wa Taasisi ya Arrayan ambayo inajishughulisha na uchinjaji, Abdul Rahmani Shaabani (kushoto) akiwajibika wakati wa uchinjaji wanyama hao kituo cha Nuru Islamic Foundation.
Askari binafsi wakiwa wameimalisha ulinzi wakati wa zoezi hilo.
Uchinjaji ukifanyika kituo cha Karakana.
Uchinjaji ukiendelea katika kituo hicho cha Karakana.
Mwonekano wa mbuzi na kondoo waliokuwa wakisubiri kuchinjwa kituo cha Karakana.
Mbuzi wakisubiri kuchinjwa kituo cha Karakana.

No comments:

Powered by Blogger.