LIVE STREAM ADS

Header Ads

WANANCHI WA LUCHELELE JIJINI MWANZA WACHACHAMAA JUU YA HATMA YA ARDHI YAO. WAPANGA KUKUTANA KESHO.



Kutokana na tatizo kubwa la migogoro ya ardhi Jijini Mwanza kukithiri katika maeneo mbalimbali, wananchi wa eneo la Luchelele Jijini hapa, wamesema hawako tayari kunyanyaswa mpaka kieleweke.

Hatua hii imekuja baada ya Halimashauri ya Jijiji la Mwanza  kutoa taarifa kwa wakazi wa eneo hilo
inayoelekeza kwamba baadhi ya maeneo yaliyopo katika eneo hilo yanatakiwa kuwekwa wawekezaji kwa ajili ya maendeleo ya Jiji la Mwanza.

Mgogoro huo unaoendelea eneo la Luchelele kata ya Mkolani Wilayani Nyamagana , umekuwa kitendawili hadi sasa kutokana na baadhi ya wananchi waliochukuliwa maeneo yao kudai kuwa muafaka hauta patikana mpaka walipwe fidia inayolingana na maeneo yao yaliyochukuliwa na halmashauri ya Jiji la Mwanza.

Mgogoro huo ulioanza tangu mwaka 2006  na kutegemewa kumalizika mwaka 2011, lakini hadi sasa hali ni tete kwa wakazi waishio maeneo hayo ambapo swala hilo bado halijapatiwa ufumbuzi huku baadhi ya maeneo yakidaiwa kujengwa na baadhi ya Viongozi wa Jiji la Mwanza.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti  juzi, wakazi wa maeneo hayo walisema kuwa tatizo hilo limeanza muda mrefu na hadi sasa hawaelewi litaisha lini na hakuna taarifa yoyote wanayoipata kutoka kwa viongozi wa juu.

‘’Hatujaona chochote kinachoendelea hapa Luchelele sisi hatuondoki kwa sababu tangu watuambie watatulipa fidia zetu ili tupishe ardhi  hii hawajafanya hivyo, sasa twende tukakae wapi na hata hizo fidia wanazosema watulipe hazilingani na maeneo yetu’’. Alisema mmoja wa wakazi wa eneo hilo.

Aliongeza kuwa  pamoja na kuchagua mwakilishi atakaye wasilisha hoja zao kwa uongozi wa halmashauri ya Jiji la Mwanza kwa ajili ya migogoro hiyo, hakuna taarifa yoyote muafaka juu ya ardhi yao na kudai kuwa hawataondoka katika maeneo hayo hadi pale swala hilo litakapo kamilika.

‘’Huyu mwenyekiti wa mgogoro tumemchagua sisi lakini sasa ametugeuka na kuwa adui yetu, hatuambii chochote kinachoendelea huko Jijini, wala hatupati taarifa yeyote sasa sisi hatuondoki hata kwa ngumi’’alisema mkazi huyo.

Wengine walieleza kwamba hawakatai  kupisha katika eneo hilo kwa ajili ya maendeleo, isipokuwa wanachokitaka wao ni kupewa ruhusa ya wao kuendelea kujenga katika viwanja vyao kwani walizuiliwa na halmashauri kutofanya shughuli za ujenzi kwa wale wanaojenga hadi pale watakapo pewa taarifa kutoka jiji Mwanza.

Kutokana na hali hyo wananchi hao wamepanga kufanya mkutano wao utakao fanyika leo Jumamosi wakiongozwa na Mwenyekiti wa mtaa wa Luchelele kati, Vicent Lusana na hivyo kuwataka  wananchi kujitokeza kwa wingi katika kikao hicho kitakachofanyika  shule ya msingi Luchelele ili kujadili muafaka wa mgogoro hu unao wakabiri.

Akizungumzia swala hili kwa njia ya simu, Meya wa jiji la Mwanza Stanslaus Mabula alikiri kuwepo kwa mgogoro huo na kudai kuwa ulikuwa umefikia mwisho lakini umeibuliwa na wanasiasa kutokana na kwamba kuna baadhi ya watu wanaotumia mgogoro huo kwa njia ya kujinufaisha kisiasa na kuwatumia wananchi kuwachochea kufanya maandamano yasiyo na tija.

Aliongeza kuwa tarehe 3 Septemba  utafanyika mkutano katika eneo hilo kwa lengo kujadili namna ya kutatua mgogoro huo ili kuruhusu wananchi wanaomiliki ardhi katika eneo hilo la Luchelele kuendelea kufanya shughuli zao za kiuchumi.
Na Prisca Japhes: Mtanzania Media-Mwanza.

No comments:

Powered by Blogger.