LIVE STREAM ADS

Header Ads

DC MPYA KINONDONI MH.PAUL MAKONDA ASEMA ATAONGOZA KWA KUFUATA SHERIA NA SI MIHEMUKO YA KISIASA.

Na: George Binagi-GB Pazzo.
Siku moja baada ya kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr.Jakaya Kikwete, Mkuu Mpya wa Wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es salaam Mh.Paul Makonda amewaondoa wananchi hofu kwa kusema kuwa uongozi wake utasimamia kanuni, taratibu na sheria na siyo mihemko ya kisiasa kama wengine wanavyonadhia.

Mh.Makonda alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na 99.4 Radio Metro Fm ya Jijini Mwanza kwa njia ya simu, akielezea namna alivyopokea uteuzi wake sanjari na kuzungumzia mijadala mbalimbali iliyoibuka katika mitandao ya kijamii kufuatia uteuzi wake.

Mh.Makonda ambae kabla ya utauzi huo alikuwa ni Katibu wa Hamasa wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Taifa, alisema kuwa jambo la kwanza anamshukuru Rais Kikwete kwa kumuamini na kumuteua kuwa msaidizi wake katika Wilaya ya Kinondoni huku pia akiwashukuru Watanzania waliomuombea na kumpa ushirikiano katika kutekeleza majukumu yake mbalimbali na hatimae kuonekana anafaa kuwa kiongozi Serikalini.

“Haki ni tofauti na dhambi. Ukiwa na dhambi hofu itakutawala. Ukiwa na haki ujasiri ni sehemu ya maisha yako. Asie kuwa na hatia na asonge mbele katika utendaji wake wa kazi. Alie na hatia hofu ndiyo itakayomtafuna. Kwa nafasi tuliyopewa tunakwenda kuifanya kazi kwa mjibu wa sheria, taratibu na kanuni.

Sasa sitegemei uwe na hofu wakati taratibu unazijua, sheria unazijua na kanuni unazijua”. Alisema Makonda wakati akijibu hoja kwa wanaodhania uongozi wake utagubikwa na mihemuko ya kisiasa.

Pamoja na mambo mengine pia Makonda alihitimisha kwa kusema kuwa hakuna Tanzania bila Mtanzania na hakuna Mtanzania bila Tanzania hivyo Watanzania hususani vijana watimize majukumu yao vyema kwa ajili maendeleo ya Taifa ambapo alishauri kuwa huu ni wakati wa kujituma, kujifunza na kubadilika na siyo wakati wa kujadili vitu au watu ambapo aliwahimiza zaidi wazee pamoja na viongozi mbalimbali wa dini kuendelea kuliombea Taifa ili lidumu katika Amani, Umoja na Utulivu kwa faida ya Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Juzi Februari 18 Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Mizengo Pinda aliweka wazi uteuzi wa Wakuu wa Wilaya uliofanywa na Rais Kikwete ambapo uteuzi huo uliwang’oa madarakani wakuu wa wilaya 19 na kuwateua wapya 27 sanjari na kuwahamisha 64 huku 42 wakibaki kwenye vituo vyao vya kazi.


Muda mfupi baada ya Uteuzi huo, ziliibuka hoja na Mijadala mbalimbali hususani katika mitandao ya kijamii ambapo watu wengi walikuwa wakizungumzia uteuzi huo ambao walikuwa wakiuelezea kuwa umeonekana kama Ahsante kutoka kwa Rais Kikwete kwa baadhi ya Wakuu wa Wilaya wapya kutokana na harakati zao za kisiasa ndani ya Chama cha Mapinduzi CCM.

No comments:

Powered by Blogger.