LIVE STREAM ADS

Header Ads

DIWANI KATA YA MKOLANI JIJINI MWANZA AAGIZA KUFANYIKA SENSA KWA WATU WENYE ULEMAVU WA NGOZI.

Na: George Binagi-GB Pazzo
Diwani wa Kata ya Mkolani (CCM) Jijini Mwanza Stanslaus Mabula amemwagiza Mtendaji wa Kata hiyo kwa kushirikiana na Watendaji wengine wa Serikali za Mitaa, kufanya Sensa kwa watoto wenye ulemavu wa ngozi kwa lengo la kuwaimarishia Ulinzi.

Mabula ambae pia ni Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza alitoa kauli hiyo juzi kufuatia kukithiri kwa vitendo vya Utekaji na Mauaji kwa watu wenye Ulemavu wa ngozi hapa nchini hususani katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa.

Alisema kuwa anasikitishwa na Vitendo vya Ukatili, Utekaji na Mauaji kwa Watoto wenye ulemavu wa ngozi katika kipindi hiki cha kuelekea katika Uchaguzi Mkuu, jambo ambalo linaongeza wasiwasi kwamba kuna baadhi ya wanasiasa wanahusika katika kufadhiri vitendo hivyo.

“Mimi niseme tu binafsi nimepokea kwa masikitiko makubwa suala hili. Hivi karibuni tumesikia Albino kule Kwimba ametekwa mpaka leo hajapatikana. Albino Geita pale ametekwa na amepatikana akiwa marehemu na baadhi ya viuongo vyake vimechukuliwa. Niseme tu mimi kama mwanasiasa lakini kama binadamu mwingine na mwananchi wa kawaida kitendo hiki siyo kizuri, kinaumiza sana na kinachukiza na hasa pale kinapoanza kuhusishwa na nyakati hizi za Uchaguzi”. Alisema Mabula na Kuongeza,

“Sisi wanasiasa hatuwezi kufanana wote na wala siwezi kusema hapana au ndiyo, inawezekana tafiti zinaonyesha wapo watu wanatumia mbinu hizo za kuwaua watu wenye ulemavu wa ngozi lakini mimi niseme tu siyo jambo zuri maana hata mwanasiasa unaeshinda kwa kumuua mwanadamu mwenzako kisa tu ualibino wake siku moja mwenyezi Mungu atakupa uongozi wa adhabu ambao daima huwezi kuufurahia katika Maisha yako”.

Kufuatia hali hiyo Mabula alibainisha kwamba pamoja na kwamba jeshi la polisi linafanya kazi kubwa ili kuhakikisha linawalinda watu wenye ulemavu wa ngozi, pia yeye kama Diwani wa Kata ya Mkolani amemwagiza Mtendaji wa Kata hiyo kwa kushirikiana na watendaji na Wenyeviti wa Mtaa kuhakikisha kwamba wanapita katika kila Kaya na kutambua walipo watoto wenye ulemavu wa ngozi kwa lengo la kuwaimarishia ulinzi ili kuongeza wigo na upana wa maisha yao kadri Mungu alivyowapangia.

Hivi karibuni katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa kumeibuka Vitendo vya Utekaji na Mauaji kwa watoto wenye Ulemavu wa ngozi jambo ambalo limeushtua ulimwengu mzima ambapo mwishoni mwa mwezi Januari akizungumza Mkoani Mwanza, Peter Ash ambae ni Mkurugenzi wa Shirika la kutetea haki za watu wenye Ulemavu wa ngozi (Under The Same Sun) lenye Makao yake Makuu nchini Canada aliitaka Serikali kuwachukulia hatua kali za kisheria watu wote wanaotajwa kufadhiri vitendo vya Utekaji na Mauaji kwa watu wenye ulemavu wa ngozi ambapo aliwatupia lawama baadhi ya Wafanyabiashara na Wanasiasa kuhusika katika kufadhiri vitendo hivyo.


Itakumbukwa kuwa Disemba 27 mwaka jana mtoto mwenye ulemavu wa ngozi Pendo Emmanuel (4) Mkazi wa Kwimba Mkoani Mwanza alitekwa na watu wasiojulikana na mpaka sasa hajulikani alipo huku tukio kama hilo likijrudia tena Februari 15 mwaka huu katika Kijiji cha Ilelema Mkoani Geita ambapo mtoto mwenye ulemavu wa ngozi Yohana Bahati (1) alitekwa akiwa amebebwa na mama yake mzazi na baada ya siku mbili akapatikana akiwa tayari ameuawa huku baadhi ya viuongo vyake vya mwili vikiwa vimekatwa. Katika tukio hilo wavamizi hao walimjeruhi vibaya kwa mabanga mama yake na Yohana wakati akijaribu kumuokoa mwanae.

No comments:

Powered by Blogger.