Kilimo cha umwagiliaji suluhisho la mabadiliko ya tabia nchi
Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Kiongozi wa skimu ya kilimo cha umwagiliaji cha Mkombilenga iliyopo wilayani Iringa katika Kanda ya Umwagiliaji ya Mbeya, Fundi Mihayo (kulia) akipokea kikombe kutoka kwa Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA) hapa nchini, Nahofumi Yamamula baada ya skimu hiyo kushika nafasi ya kwanza katika kongamano kubwa la kushindanisha vyama vya umwagiliaji lilofanyika jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mbogo Futakamba akitoa neno la kufunga kongamano hilo lililoshindanisha vyama wa umwagiliaji jijini Dodoma.
Majaji na washiriki wakiwa kwenye kongamano la siku mbili la kushindanisha vyama vya umwagiliaji lililofanyika jijini Dodoma.
Mwakilishi Mkazi wa Shirika la kimataifa la maendeleo la Japan (JICA) nchini, Nahofumi Yamamula (katikati) akiongea na Katibu Mkuu mstaafu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mbogo Futakamba (kushoto) baada ya mapumziko wakati wa kongamano la kushindanisha vyama vya umwagiliaji lilofanyika jijini Dodoma. Kulia ni Yoichi Yamauchi Mshauri kutoka mradi wa kuwajengea uwezo wakulima katika eneo la umwagiliaji.
Na Mwandishi Maalum, Dodoma
Kuwekeza katika kilimo cha umwagiliaji
kunaweza kuwa ni njia sahihi ya kuhimili athari zitokanazo na mabadiliko ya
tabianchi.
Hayo yamesemwa jijini Dodoma na Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya
Maji, Mhandisi Mbogo Futakamba alipokuwa akifunga kongamano ya wakulima
lililoandaliwa na shirika la Maendeleo la kimataifa la Japan (JICA) kwa
kushirikiana na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji.
Mhandisi Futakamba alisema Serikali
imeweza kuwekeza kwa kiasi kikubwa katika miundombinu ya Umwagiliaji na
kuchukua jukumu kubwa la kutoa mafunzo ya matunzo ya miundombinu hiyo kwa
wakulima, ili kuweza kukabiliana na athari na hasara zitokanazo na mabadiliko
ya tabianchi,
"Ili kuweza kufikia lengo hili ni lazima serikali na wakulima
kwenda pamoja ili kufanikisha, hali ambayo inaweza pia kusaidia wakulima nao
kuingia zaidi katika kilimo cha biashara kama vile wakulima wa skimu ya Lemkuna
na Pawaga, pamoja na kuwa na uhakika wa chakula nchini" alisema Mhandisi
Mbogo.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa
Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Marco Ndonde alisema Tume hiyo imejipanga
kuboresha miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji kwa kushirikiana na wadau
mbalimbali ikiwemo benki ya kilimo na mashirika mbalimbali ya maendeleo.
"Sambamba na hilo Tume ina mpango wa kujenga mabwawa ili kufanya kilimo cha
umwagiliaji kiwe na uhakika wa kupata
maji ya kutosha pamoja na kufungua miradi ya kilimo hicho kitakachoajiri vijana
kutoka vyuo vikuu nchini" alisisitiza Ndonde.
Akiwasilisha mada katika siku ya
mwisho ya kongamano lililoshindanisha vyama vya wamwagiliaji nchini, Fundi
Mihayo ambaye ni kiongozi wa skimu ya umwagiliaji ya Mkombilenga iliyopo mkoani Iringa
alisema lengo la Serikali kuwezesha wakulima kuuza mchele badala ya kuuza
mpunga katika maeneo ya skimu za kilimo cha umwagiliaji limefanikiwa kwa kisia
kikubwa kwani kwa sasa skimu nyingi zimeweza
kufunga mashine za kukoboa nafaka kama vile mpunga na kupaki katika
madaraja na ujazo tofauti.
"Haya yote ni manufaa ya tokanayo na serikali
ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kutoa mafunzo kwa kushirikiana na serikali
ya Japan kupitia shirika lake la JICA jambo ambalo limepelekea wakulima kuwa
na soko la uhakika la zao la mpunga hasa baada ya Serikali kuhamia Makao Makuu
ya nchi Dodoma, wakulima wa skimu ya
umwagiliaji Mkombilenga wamepata soko la uhakika Jijini Dodoma" alisema Mihayo.
Wakitoa mawasilisho kwa baadhi ya
skimu za umwagiliai zilizopo katika kanda nane (8) za umwagiliaji nchini,
wakulima wameonekana kutaja changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo katika skimu hizo ikiwa ni pamoja na kuwepo
kwa hitaji la kuongeza mifereji
inayopeleka maji katika skimu hizo pamoja na kuisakafia na kuishauri Serikali
kuendelea kutoa mafunzo kwa skimu zote ili wakulima wapate uelewa na kutunza
skimu jambo ambalo linaweza kusaidia Serikali kufikia lengo la kuweza kuongeza
kipato kwa wanachi na kuwepo kwa uhakika wa chakula.
Skimu ya umwagilijai ya Mkombilenga iliyopo katika Kanda ya Mbeya
imeibuka kidedea ikifuatiwa na skimu ya Lemkuna ya Kanda ya Dodoma na skimu ya
Nyida iliyopo katika Kanda ya Mwanza kushika nafasi ya tatu katika mashindano
hayo.
Kongamano hilo la siku mbili
lilishirikisha wakulima, wataalam wa kilimo kutoka ngazi za Mikoa, Wilaya, Kanda
za Umwagiliaji, Tamisemi na Ofisi za Tume ya Umwagiliaji.
No comments: